Wizara ya Fedha na Mipango imesema kuwa kampuni ya Pride ipo kwenye hatua za ufilisi baada ya Ofisi ya Msajili wa Hazina kuagizwa kusimamia suala hilo
Aidha, madai yoyote yanayohusu kampuni hiyo yatashughulikiwa kwa kufuata taratibu za ufilisi.
Naibu Waziri, Hamad Yusuf Masauni, aliyasema hayo bungeni jana alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mtwara Mjini (CCM), Hassan Mtenga.
Katika swali lake, Mtenga alihoji lini serikali itashughulikia urejeshwaji wa fedha za wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini ambao walijiunga na Pride kwa ajili ya kupata mkopo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Masauni alisema kulikuwa na shauri mahakamani lililofunguliwa mwaka 2016 kuhusu umiliki wa kampuni ya Pride.
“Baada ya kukamilika kwa shauri hilo na kutolewa hukumu tarehe 11 Novemba, 2018 kuwa kampuni ya Pride Tanzania ni mali ya serikali,” alisema.
Hata hivyo, alisema serikali ilifanya tathmini ya hali ya kampuni na kufuatiwa na ukaguzi maalum uliofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kutambua mali na madeni ya kampuni hiyo ambapo taarifa ilionyesha kuwa kampuni ina madeni makubwa kuliko mali zilizopo.