Moshi. Polisi Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro nchini Tanzania limevamia mkutano wa ndani wa Mbunge wa Hai (Chadema), Freeman Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni nchini humo.
Polisi hao wakiongozwa na mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD), Lwelwe Mpina wamevamia mkutano huo leo Jumatatu Septemba 30,2019 kwa maelekezo ya mkuu wa wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya.
Sabaya amethibitisha kutuma polisi hao akisema amefanya hivyo kwa ajili ya kuhakikisha usalama wa Mbowe na viongozi wengine pamoja na wananchi, akisema hawana sababu ya kutaharuki kama ni raia wema.
"Mkutano wa chama cha siasa sio send off au harusi. Mkutano wa chama cha siasa polisi wana haki ya kuwepo. Hata mikutano ya CCM polisi wanakuwepo. Tunafuatilia agenda ni nini hasa," amesema Sabaya ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo.
Polisi walifika katika ofisi za Chadema wilaya ya Hai na kulazimisha kuingia ndani ya mkutano huo ili kujua nini kinachozungumzwa kwa lengo la kusimamia ulinzi na usalama kwao na kwa wananchi.
Mkutano huo bado unaendelea na polisi wako ndani na wengine wako nje.
Pia Soma
- Watoto wa miaka minne Ghana kufundishwa elimu ya uzazi
- Trump ataka kukutana na mtu aliyetoa siri dhidi yake
- Mkurugenzi Airtel Tanzania aaga wafanyakazi, aishukuru Serikali
- Matumizi ya noti ya Sh1,000 mwisho leo Kenya