Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Ntunzwe: TRA hawajatekeleza agizo la Rais, wenyewe wajitetea

99814 Ntunwe+picc Ntunzwe: TRA hawajatekeleza agizo la Rais, wenyewe wajitetea

Thu, 26 Mar 2020 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Dar es Salaam. Takriban miezi minane, tangu Rais John Magufuli alipotoa agizo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), kumlipa fidia Ramadhani Ntunzwe wa Dar es Salaam baada ya kumsababishia hasara, mfanyabiashara huyo amelalamika kuendelea kuzungushwa.

Hata hivyo uongozi wa TRA umesema bado unafanya mashauriano na mfanyabiashara huyo na kwamba mashauriano hayo ni siri baina yake na Ntunzwe.

Tangu wakati huo, Ntunzwe anasema amefuatilia fidia hiyo bila mafanikio huku akidai kwamba Kamishna Mkuu wa TRA, Edwin Mhede amemwambia awape muda zaidi. Pia mfanyabiashara huyo alisema amekuwa akizungushwa na hadi sasa suala lake halijapata ufumbuzi.

Sakata la Ntunzwe linaanzia 2017 alipokuwa akisafirisha mzigo wake kutoka Zambia kupitia mpaka wa Tunduma. Baada ya kufika Mbezi, Dar es Salaam, alikamatwa na maofisa wa TRA waliomdai rushwa ya Sh2 milioni lakini alikataa kuwapa fedha hizo.

Baadaye suala hilo lilichukua sura mpya baada ya maofisa hao wa TRA kumbambikia makosa ya kukwepa kodi na hatimaye kutaifisha mali zake, huku nyingine zikiharibiwa na kuporwa fedha taslimu kiasi cha Sh60 milioni.

Ntunzwe anadai kuwa hasara ya kutaifishwa na kuharibiwa mali zake katika jaribio la mali hizo kupigwa mnada na kuibiwa kwa fedha taslimu, vilimsababishia hasara inayofikia Sh821 milioni.

Pia Soma

Advertisement
Wiki iliyopita Mwananchi lilizungumza na Naibu Kamishna Mkuu, Msafiri Mbibo na alipoulizwa kuhusu suala hilo alisema; “Mimi nikuombe mtafute yeye (Ntunzwe) ili akupe maelezo yake halafu kama ana jambo atakuja kwangu.”

Hata hivyo, alipoambiwa na mwandishi wa gazeti hili kwamba alishazungumza na mhusika, alikata simu.

Baadaye alipatikana Mkurugenzi wa Elimu kwa Mlipakodi wa TRA, Richard Kayombo ambaye alipoulizwa kuhusu maagizo ya Rais kwa taasisi yake alisema: “Suala hilo tunalifanyia kazi ndani ikiwa ni pamoja na kuongea na mfanyabiashara huyo. Hatutoi taarifa kwa vyombo vya habari.”

Katika maagizo yake kuhusu suala la Ntunzwe, Rais Magufuli pia aliiagiza Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) kuwakamata wahusika wote waliombughudhi mfanyabiashara huyo na kumsababishia hasara hiyo, jambo ambalo lilitekelezwa.

Juni 9, 2019 Ofisa Msaidizi wa Kodi wa TRA, Charity Ngalawa (28) na askari polisi wawili walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu shtaka la kuomba rushwa ya Sh2 milioni kutoka wa Ntunzwe.

Mbali na Ngalawa washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya jinai ni polisi Ramadhani Uweza (28) na mwenzake Simon Sugu (26), wote wa Kituo cha Polisi Osterbay, wilaya ya Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Wakili wa Takukuru, Sofia Gula alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, kuwa washtakiwa kwa pamoja walitenda kosa hilo Oktoba 29, 2016 katika eneo la Kimara Mwisho, Wilaya ya Kinondoni.

Maelezo mapya

Akizungumza mwishoni mwa wiki iliyopita, Ntunzwe alisema siku tatu baada ya agizo la Rais Magufuli alikutanishwa na maofisa wa TRA na mmoja wa viongozi wa Jumuiya ya wafanyabiashara (jina tunalihifadhi).

Alisema walipanga kuonana na maofisa hao, Juni 9, 2019 lakini ilishindikana wakapanga kesho yake, Juni 10 na kukutania Hoteli ya Tiffany Diamond, mtaa wa Jamhuri katikati ya jiji la Dar es Salaam. Alisema alichukua tahadhari kwani alihofia usalama wake.

Alisema alikutana na mmoja wa maofisa wa TRA (jina pia linahifadhiwa) kwa saa nne, ambaye alimshawishi akubali kulipwa fedha zake kwa siri, lakini yeye (Ntunzwe) alilikataa.

“Nikauliza, hiyo siyo pesa ndogo, mkinipa nitaiweka wapi? Nikiipeleka benki nitasema nimeitoa wapi? je, nikiiweka ndani hamwoni kwamba mtanihatarishia maisha kwa sababu majambazi yanaweza kuja kuniua ili waichukue? Nikawaambia mimi sijaafiki,” alisema Ntunzwe.

Alisema kikao hicho kilivunjika bila kupata mwafaka na hata walipomwomba kukutana baada ya siku nne, alikataa.

Arudi TRA

Alisema Juni 22, 2019 alimwandikia barua Kamishna Mkuu wa TRA, akimkumbushia madai yake kama Rais alivyoelekeza.

“Niliipeleka barua hiyo kwa mkono na nikiwa pale ofisini kwake alimwita Naibu Kamishna Mkuu, Mbibo na kunikabidhi kwake. Akamwagiza ashirikiane nami kuhakikisha nalipwa fedha zangu. Naibu kamishna alinipeleka ofisini kwake na kuahidi kunisaidia,” alisema Ntunzwe.

Alisema Julai 16, 2019 walikaa kikao cha kwanza na Mbimbo aliyekuwa pia na Kamishna wa kodi za ndani na meneja wa kodi wa Mkoa wa Ilala ambapo aliwasimulia sakata zima, kisha waliahidi kushughulikia madai yake na kutoa ripoti Julai 30, 2019. Hata hivyo alisema baada ya hapo hakushirikishwa lolote.

Alisema Agosti 25, 2019 alifika ofisini kwa Mbibo ambaye alisema ameipa timu nyingine kulifanyia kazi suala hilo na kwamba timu hiyo itafika dukani kwake Septemba 4.

Ntunzwe alisema timu hiyo ilipofika aliisimulia mkasa mzima nao waliahidi kufuatilia na kwamba Septemba 19, 2019 walimpigia simu wakimtaka kesho yake afike ofisini kwao saa 3 asubuhi.

“Nilipokwenda walisema waliomba ripoti ya fedha zangu kwa benki zote Tanzania. Ndipo benki ya Azania ikawapa taarifa zangu zikionyesha kuwa wakati mgogoro wangu unaanza na TRA nilikuwa na Sh278.7 milioni na kwamba mwaka 2017 nilikuwa na Sh137.7 milioni,” alisema Ntunzwe na kuongeza:

“Walisema eti kutokana na taarifa za benki wameona TRA wanilipe Sh137.7 milioni kama inavyoonyeshwa kwenye kumbukumbu ya benki”. Alisema alipotakiwa atoe maoni yake, alihamaki akisema haihusiani na madai yake ambayo Rais Magufuli aliagiza yashughulikiwe. Alisema pia kikao hicho kilivunjika.

“Oktoba 2019 niliendelea kufuatilia suala hilo, kila nikifika kwa Naibu Kamishna mkuu anasema bado linashughulikiwa na kwamba Novemba 2019, alimpigia tena simu kumuuliza.

“Mbibo alisema ripoti yangu imeshakamilika na imepelekwa Hazina kwa ajili ya malipo. Nikamuuliza, imekuwaje ripoti yangu iende Hazina wakati mimi sijaiona? Je, nitajuaje kama nalipwa Shilingi ngapi? Kama mimi ni mhusika mbona sijasaini?” Alisema Ntunzwe.

Alisema aliendelea kufuatilia suala lake kwa Mbibo na kumweleza kutoridhishwa na jinsi mambo yanavyokwenda na kumwomba amrudishe kwa Kamishna Mkuu, Mhede.

“Februari 24, 2020 nilimwandikia ujumbe Mhede nikimweleza hatua zote nilizopitia kwa miezi minane bila mafanikio. Nikamwambia narudi kwake ili anipe jibu.

Alisema baada ya kutuma ujumbe huo alipigiwa simu na mtu aliyesema ametumwa na Mhede akisema kesho yake nifike ofisini kwake kutakuwa na kikao changu.

Alisema kesho yake hawakuweza kukaa kikao bali aliendelea kupigwa kalenda hadi Jumanne Machi 10 alipofanikiwa kukutana na Mhede.

“Nikamweleza kuhusu kikao cha Septemba 24 nikasema sikuridhishwa nacho. Baada ya kunisikiliza naye akasema nilifanya makosa kutopokea ile fidia ya Sh137.7 milioni. Akasema nilipaswa kuipokea kwanza wakati naendelea kudai.

“Alisema unajua ukiwa na njaa usikatae chakula, ni bora uchukue. Mimi nilikataa nikasema siwezi kuichukua kwa sababu siyo haki yangu ninayodai,” alisema.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live