Kigoma. Norway imetoa Sh9.9 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo inayozunguka kambi za wakimbizi mkoani Kigoma nchini Tanzania kupitia mpango wa pamoja wa Kigoma (KJP).
Akizungumza leo Jumanne Februari 4, 2020 mjini Dodoma katika mkutano wa nne wa utaratibu wa kushirikiana na Umoja wa Mataifa na nchi rafiki ambazo zinasaidia KJP, mshauri wa masuala ya kisiasa wa ubalozi wa Norway nchini Tanzania, Hans Corneliussen amesema fedha hizo ni kwa ajili ya kusaidia wananchi wa Mkoa huo.
Amesema wataendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania kuinua uchumi wa Mkoa huo hasa jamii inayozunguka wakimbizi.
Awali, akifungua mkutano huo mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Brigedia Jenerali mstaafu Emmanuel Maganga amesema mpango wa KJP umeleta mabadiliko makubwa mkoani Kigoma.
Amesema mambo yanayooneka katika mpango huo ni pamoja na kuimarika kwa sekta ya afya, elimu pamoja na miundombinu na kujengwa kwa masoko.
"Mpango huu wa KJP umesaidia kuinuka uchumi katika Mkoa wetu wa Kigoma, wananchi wangu wakipata maendeleo watashirikiana vizuri na wakimbizi kwa wakati huu wakiwa bado nchini kwetu, "amesema Maganga.
Pia Soma
- Mbunge CUF awatuhumu polisi kuwapiga wapinzani, Masauni amjibu
- Daftari la wapigakura kukamilika mwezi huu
- Wabunge Tanzania wataka wabakaji wahasiwe, AG awatetea
Amesema mpango huo upo katika eneo la afya, maji, kilimo, elimu, eneo la kuwezesha wanawake na uchumi , kutokomeza unyanyasaji dhidi ya kina mama na watoto na eneo la nishati na mazingira.
Amesema fedha hizo zitaenda kutekeleza maeneo manne ya mradi huo ambayo ni kilimo, Maji, eneo la kutokomeza vitendo vya unyanyasaji dhidi ya kina mama na watoto na eneo la kuwezesha kina mama na vijana kiuchumi.