Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Nitamsindikiza Hasunga kuapishwa Dodoma-Mkisi

56fa96f4f2b3867f744237f4e3660163 Nitamsindikiza Hasunga kuapishwa Dodoma-Mkisi

Mon, 28 Sep 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MGOMBEA Ubunge Jimbo la Vwawa kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Fanuel Mkisi, amesema atamsindikiza Dodoma kwenda kuapishwa Mgombea Ubunge wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) katika jimbo hilo, Japhet Hasunga kama atashinda kwa haki.

Hasunga ni mbunge aliyemaliza muda wake ambaye anachuana na Mkisi kwa mara ya pili katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu. Akizungumza juzi na wananchi wa Kata ya Kilimapimbi kwenye mkutano wa kampeni, alisema safari hii endapo atakusanya matokeo katika vituo vya kupigia kura, ikaonekana ameshinda, ana imani wahusika watamtangaza bila kuweka figisu.

“Endapo mwenzangu Japhet Hasunga atakuwa ameshinda kwa haki nitamuunga mkono na nitamsindikiza Dodoma kuapishwa, maana sisi sote ni wana Vwawa, tunajenga nyumba moja, hatutakiwi kugombea fito, atakayeshinda tutamuunga mkono ili aweze kutimiza ahadi zake,”alisema.

Akizungumzia huduma za afya, aliwaahidi wananchi kuwa mara tu atakapochaguliwa, atakwenda kuonana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto ili asaidie kuleta wahudumu wa afya, wauguzi na madaktari katika zahanati ya Kilimapimbi.

Alisema zahanati hiyo ambayo ilijengwa kwa mamilioni ya fedha zikiwemo zilizochangwa na wananchi, haina wahudumu wa afya kwa miaka mitano sasa na hivyo wananchi wanakosa huduma za afya.

Kuhusu michango michango, alisema akichaguliwa wananchi hawatatozwa michango zaidi ya Sh 3,000 kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Mkisi alisema inashangaza hivi sasa wananchi wanatozwa michango mikubwa kuanzia Sh 20,000 bila kujali kuwa kipato chao ni kidogo.

Chanzo: habarileo.co.tz