Bariadi. Ng’ombe mwenye kilo 643 amegeuka kivutio kwenye maonyesho ya wakulima maarufu ‘Nanenane’.
Katika banda la Kampuni ya Ranchi za Taifa (Narco) lililopo viwanja vya Nyakabindi wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu, yumo dume la ng'ombe aina ya Boran anayeitwa Matonya mwenye uzito wa kilo 643.
Upekee wa Matonya, ambaye asili yake ni nchi za Kenya na Ethiopia siyo tu ukubwa wa umbo na uzito pekee, bali hata bei siyo ya kawaida kulinganisha na mifugu ya jamii za wafugaji nchini kwani anauzwa Sh4 milioni.
Ng'ombe huyo mwenye umri wa miaka mitatu, ana thamani zaidi ya mara tano ukilinganisha na madume wengine wa rika lake wasiyo wa asili ya Boran wanaouzwa kati ya Sh500, 000 hadi Sh600, 000.
Jumanne Karim, mmoja wa wasimamizi wa banda la Narco amewataka wafugaji nchini kubadilisha aina ya mifugo yao ili kupata tija.
"Wafugaji wanaweza kubadilisha mifugo yao kwa kununua madume ya Boran yanayopatikana katika ranchi za Taifa," amesema Karim.
Mmoja wa wafugaji waliotembelea banda la Narco, Jonson Masanja ameiomba Serikali kusambaza elimu ya ufugaji wenye tija kwa wafugaji vijijini badala ya kusubiri maonyesho na matukio maalum.
"Hawa wataalam watutembelee vijijini kutuelimisha namna bora ya kubadilisha aina ya mifugo ili sekta ya ufugaji uwe na tija na kuchangia maendeleo ya Taifa," ameshauri Masanja
Tanzania ni nchi ya tatu kwa wingi wa mifugo barani Afrika ikitanguliwa na Ethiopia na Sudan.
Mkoa wa Simiyu ndio wenye idadi kubwa ya mifugo nchini ikimiliki asilimia 40 ya mifugo yote nchini.