Arusha. Kufuatia maduka ya kubadilisha fedha za kigeni jijini hapa kufungwa kufuatia uchunguzi wa Benki Kuu (BoT), neema imezishukia benki za biashara kwa kuanza kupokea wateja wapya.
Mwananchi limeshudia wateja hao katika moja ya benki iliyopo mtaa wa Clock Tower wakipata huduma baada ya kukuta maduka waliyozoea kubadilisha fedha yakiwa yamefungwa.
Ofisa wa benki hiyo ambaye hakupenda jina lake liandikwa gazetini kwa kuwa si msemaji wa benki hiyo alisema idadi ya wateja imeongezeka tofauti na siku zilizopita.
"Siwezi kuzungumzia zaidi, wapo wakubwa zetu makao makuu jijini Dar es Salaam wanaweza kutoa takwimu sahihi," amesema.
Hata hivyo amekiri kuwa wateja wengi huwa hawapendi kupata huduma ya kubadilisha fedha za kigeni kwenye mabenki kutokana na gharama za kununua na kuuza kutowafurahisha wateja wengi.
Katika tawi la benki jirani hali ilikua hivyo hivyo wakipokea wateja wapya na kutokua tayari kuzungumzia hali hiyo.
Mmoja wa wateja aliyejitambulisha kwa jina la Godfrey Mbisse amesema amelazimika kubadilisha fedha chache za kigeni kukidhi mahitaji yake huku akisubiri maduka hayo kufunguliwa tena ambayo alisema yana bei nzuri ukilinganisha na benki.