Mwanza. Watumiaji wa mitandao ya simu za kiganjani wataanza kupata nafuu ya kupiga simu katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) baada ya Serikali ya Tanzania kuanza mchakato wa kutekeleza mkataba wa EAC wa kuoanisha gharama hizo miongoni mwa nchi wanachama.
Akizungumza jijini Mwanza leo Jumatatu Julai Mosi, 2019, Naibu Waziri Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wa Tanzania, Atashasta Nditiye amesema mchakato huo utakamilika muda wowote kuanzia sasa.
Naibu Waziri huyo alikuwa anafungua mkutano wa siku tano wa wataalam wa mawasiliano kutoka mamlaka za mawasiliano za wanachama wa EAC.
Tanzania na Burundi ndizo nchi pekee kati sita wanachama wa EAC ambao hawajakamilisha mchakato huo.
Nchi za Kenya, Rwanda, Uganda na Sudan Kusini tayari zimeoanisha gharama za simu ikiwa ni utekelezaji wa mkataba wa EAC kuhusu sekta ya mawasiliano ya simu.
"Tuko hatua za mwisho kukamilisha mchakato wa kuoanisha gharama za kupiga simu miongoni mwa nchi wanachama wa EAC," amesema Nditiye
Pia Soma
- Dawasa kusaini miradi mikubwa ya kimkakati kesho
- Samia kufungua maonyesho ya 43 ya sabasaba
- Mikoa minane kusini Tanzania yashirikiana kutangaza utalii
Amesema sababu zinahusisha huduma na manufaa kwa asilimia 94 ya wananchi wote hadi vijijini.
"Sera za Tanzania ndizo zimeigwa na EAC kutokana na ubora wake na upatikanaji wa mawasiliano vijijini," amesema Kilaba
Kwa upande wake, Mtendaji wa Shirika la Mawasiliano wa EAC, Ally Simba amesema lengo la kuoanisha gharama za mawasiliano miongoni mwa raia wa nchi wanachama kurahisisha mawasiliano.