Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amezitaka kampuni za simu za mkononi nchini kuwa na utaratibu wa kukopesha wananchi simu za kisasa kwa bei rahisi ili kuchochea ukuaji wa uchumi.
Alisema serikali inataka kupitia utaratibu huo ili kila mwananchi amiliki simu hizo badala ya kuendelea kutumia simu za ‘vitochi’.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Katuka kilichopo Kata ya Msanzi wilayani hapa jana baada ya uzinduzi wa mnara wa simu wenye teknolojia ya 3G+, alisema utaratibu huo utaleta mapinduzi ya mawasiliano nchini kwa kila mwananchi kumiliki simu za kisasa na hivyo kukuza uchumi.
“Kampuni hizo za simu zinaweza kuanza na wananchi wachache kwa majaribio.... lakini niwatahadharishe na nyie wananchi muwe wastaarabu mlipe. Watakaofanya ujanjaujanja wa kukwepa kulipa simu zao zitafungiwa na kuwa ‘toys’,” alisema.