Dodoma. Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdalah Ulega amesema si sahihi watanzania kula nyama ya kuku siku za sikukuu tu.
Ulega ameyasema hayo leo Agosti 29 wakati wa hafla ya Waziri Mkuu Mstaafu, Mizengo Pinda ya kukabidhi vifaranga 3000 wa kuku chotara aina ya kuroiler kwa chama cha wafugaji wa kuku bora Dodoma (Chawakubodo)
Amesema wengi wanakula nyama ya kuku siku za sikukuu kutokana na kile wanachodai kuwa ulaji wa nyama hiyo ni anasa.
"Wengi wanakula nyama ya kuku siku ya Pasaka, Kipaimara, chistmasi, Eid na siku nyingine, halafu watu hao ndio wanaoongoza kula nyama ya ng'ombe," amesema.
Amesema kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa ulaji wa nyama ya kuku unaongoza Tanzania kuliko nyama nyingine.
Pia amewataka watanzania kuachana na fikra potofu kuwa mahindi yanayoelekea kuharibika ndiyo yanayofaa kutumika kwa mifugo hususani kuku.
Amesema kuwa mifugo inatakiwa kulishwa mahindi yenye ubora zaidi ili kupata mifugo bora zaidi.
“Kama mfugaji anahitaji kupata mifugo iliyo bora ni lazima kuithamini kwa kuipatia chakula kilichobora,” amesema.
Kwa upande wake aliyekuwa Waziri Mkuu Mzengo Pinda amesema kuwa wafugaji wa kuku nchini wanakabiliwa na tatizo la upatikanaji wa vyakula vya kutosha.
Amesema kuwa wafugaji hao pia wanakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa vifaranga bora.