Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

NBC yatoa mikopo ya trekta kwa wakulima

A53acc3bd9acb7c3455b036d6518f8cf.PNG NBC yatoa mikopo ya trekta kwa wakulima

Sat, 2 Jul 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) imezindua rasmi huduma ya utoaji wa mkopo wa treka kwa wakulima katika mkoani Ruvuma na mikoa ya jirani kwa lengo la kuwawezesha kuboresha shughuli za kilimo katika ukanda huo.

Mkopo huo ambao ni sehemu ya huduma ya ‘NBC Shambani’, unatolewa kwa masharti nafuu ambapo mteja atalipa asimilia 25 tu ya mkopo mzima kama malipo ya awali na kiasi kilichobaki atalipa kwa kipindi cha mwaka mmoja hadi mitano kulingana na makubaliano.

Akikabidhi moja ya treka kwa mteja wa kwanza kupata huduma hiyo, Katibu Tawala Msaidizi Mkoa wa Ruvuma, Bakari Ally Mketo aliipongeza NBC kwa kuanzisha huduma hiyo ambayo itawawezesha wakulima kupata matrekta kwa urahisi zaidi na kusaidia katika kuongeza uzalishaji mkoani humo.

Mkoa wa Ruvuma ni moja kati ya mikoa inayochangia kwa kiasi kikubwa katika uzalishaji wa mazao ya chakula nchini hivyo huduma hiyo itawawezesha wakulima kuboresha kilimo na kufanya sekta hiyo kuongeza tija zaidi nchini.

Kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mkoa huo una jumla ya hekta 4,007,746 za ardhi inayofaa kwa kilimo ambapo katika kipindi cha miaka mitano 2015/2020 mkoa umeweza kuzalisha tani 8.5 za mazao hadi kufikia mwaka 2020.

Meneja wa Tawi la NBC Songea, Frank Kiranga alisema huduma hiyo ni mahususi kwa wakulima wa mararaja yote mkoa wa Ruvuma na mikoa jirani ambayo madhumuni yake makuu ni kuongeza ufanisi wa shughuli za kilimo mkoani humo.

“Ili kupata huduma hii, mteja atatakiwa kuwa na shamba kuanzia hekari moja ambalo lina hati ya kimila au hati ya Kamishna wa Ardhi au mkataba wa mauziano. Pili, mteja atatakiwa kulipa malipo ya awali ya asilimia 25 na kiasi kilichobaki atalipa kwa awamu kuanzia mwaka mmoja hadi miaka mitano,” alisema.

Chacha Marwa Mwikwabe ambaye amekuwa wa kwanza kupata huduma hiyo aliishukuru NBC kwa kuanzisha huduma hiyo ambayo imemuzesha kutimiza ndoto ya kumiliki trekta na kwamba itamuongezea kasi ya uzalishaji katika shughuli zake.

Treka moja lina thamani ya Sh 62 Milioni na asilimia 25 ni sawa na Sh 15.5 milioni kama malipo ya awali.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live