Dar es Salaam. Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Charles Mwijage anatarajia kufungua kliniki ya biashara leo Julai 3, 2018 kwenye maonyesho ya biashara ya kimataifa (DITF) yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere Barabara ya Kilwa jijini Dar es salaam.
Waandaji wa kliniki hiyo ni Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) kwa kushirikiana na taasisi za umma na binafsi zinazoshughulikia masuala ya biashara katika sekta mbalimbali.
Kliniki ya Biashara ni kituo cha uchunguzi na utatuzi wa changamoto na matatizo yanayoikabili sekta ya biashara na kuyatafutia suluhisho la kudumu.
Lengo la kliniki hiyo ni kusaidia ukuaji endelevu wa biashara na kuimarisha mazingira wezeshi ya biashara.
Huduma zitakazotolewa kwenye kliniki hiyo ni pamoja na uchunguzi wa afya ya biashara, uchunguzi wa viashiria na changamoto zinazoikabili biashara.
Huduma nyingine ni kutoa usaidizi wa kitaalamu kwa njia ya mafunzo, ushauri elekezi, semina na kukutanishwa na waliofanikiwa.
Nyingine zitakazotolewa katika kliniki hiyo ni kushika mkono kampuni na kuipa usaidizi wa kitaalamu wa kupata teknolojia, mitaji, leseni, viwango, masoko ya ndani na nje, ubunifu wa bidhaa na taratibu za kodi.