Dar es Salaam. Changamoto ya uhaba wa hoteli za hadhi ya nyota tano katika maeneo ya vivutio vya utalii inaelekea kupatiwa ufumbuzi nchini Tanzania baada ya mwekezaji kutoka China kuonyesha nia ya kujenga hoteli tano za hadhi hiyo.
Mwekezaji huyo, Yiming Xu ambaye ni mwenyekiti wa kampuni ya Puluco China Investment tayari ameanza taratibu za kujenga hoteli Serengeti na yuko tayari kujenga nyingine nne.
Mwenyekiti wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Jaji mstaafu Thomas Mihayo amesema tayari mwekezaji huyo amewasili nchini kwa ajili ya kuangalia maeneo anayoweza kujenga hoteli hizo za kifahari.
Amesema Xu ni miongoni mwa wadau 117 wa sekta ya utalii waliokutana na TTB nchini China walipokwenda kwenye ziara ya utangazaji Juni, 2019.
Jaji Mihayo amesema mwekezaji huyo kupitia kampuni yake inayomiliki hoteli za kitalii katika mataifa mbalimbali duniani hutumia hoteli hizo kuwapeleka watalii katika nchi husika.
“Katika mazungumzo yetu na kampuni yake Xu amesema yuko tayari kujenga hoteli hapa nchini na tayari yeye na timu yake wameungana na watendaji wa taasisi za wizara ya maliasili wanamtembeza kuangalia maeneo,”
Pia Soma
- Usajili kwa alama za vidole unavyotishia kampuni za simu
- MIAKA 20 BILA NYERERE: Maisha ya utotoni ya Kambarage Nyerere-1
- Mtuhumiwa kesi ya teleza ayakana maelezo adai alilazimishwa kusaini
Jaji Mihayo ameeleza kuwa mwekezaji huyo ameeleza kuwa akipata maeneo hayo ataanza ujenzi kwa pamoja ili zikamilike zote na zianze kufanya kazi.
“Kwa kuwa lengo lake watalii watakaokuja wakae si chini ya siku 10 ni lazima awatengenezee hoteli katika vivutio ambavyo vitapendwa kutembelewa na wengi. Kati ya hizo moja itakuwa jirani na uwanja wa ndege wa Kilimanjaro ili wageni wake wakifika wapumzike,”
Pia, mwenyekiti huyo ameeleza kuwa watalii 1000 kutoka Israel wanatarajiwa kuwasilini nchini Oktoba, 2019.
Amesema watalii hao watakaokuja kwa makundi wataanza kufika Oktoba 5, 2019 na watatembelea Serengeti, Zanzibar, Ngorongoro na maeneo mengine ya vivutio.