Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Msisubiri wateja waje, wafuateni walipo - Waziri Amina Salum

AMINA SALUM TanzaniaWeb

Tue, 31 Jul 2018 Chanzo: --

WAZIRI wa Biashara na Viwanda, Balozi Amina Salum Ali, amewataka wajasiriamali Zanzibar, kuchangamkia fursa zinazotolewa ili waweze kujiendeleza kibiashara sambamba na kujitangaza kimataifa.

Ametoa changamoto hiyo alipokuwa akizindua mafunzo juu ya biashara kwa mtandao kwa wajasiriamali yaliyofanyika hoteli ya Park Hyatt, Shangani mjini Unguja jana.

Mafunzo hayo yaliandaliwa na kampuni ya usafirishaji wa mizigo na vifurushi, DHL, Tanzania.

Amesema, dunia imebadilika ambapo biashara inafanywa hata kupitia simu za mikononi, hivyo ni lazima wajasiriamali waendane na mabadiliko hayo ili kuongeza ajira na kipato.

Amesema, nchi nyingi zimefanikiwa kupitia ufanyaji wa biashara kimtandao na wajasiriamali wa Zanzibar sasa wataipata fursa hiyo kupitia kampuni ya usafirishaji wa mizigo na vifushi ya DHL Tanzania.

"Huko ndiko tunapokwenda, si wakati wa kusubiri mteja akufikie dukani au nyumbani, wajasiriamali wetu waendane na wakati ikizingatiwa mteja ni mfalme, lazima umfuate alipo," amesema.

"Soko la kufuatwa nyumbani halisaidii, tunataka kupeleka bidhaa zetu duniani na DHL imefanikiwa kwa hili. Tunachotaka ni kuwabadilisha wafanyabiashara na wajasiriamali kuwa wenye upeo wa utafutaji wa masoko, fursa zipo nyingi," amesema.

Balozi Amina, alisema Zanzibar imejaaliwa kuwa na bidhaa nyingi nzuri zinazoweza kuingizwa kwenye soko la kimataifa, kinachokosekana ni vitu vichache katika kujitangaza.

"Tunazo bidhaa nyingi za viungo ambazo iwapo wajasiriamali watafanikiwa kuzifikisha katika ubora, soko lake litakuwa la kufanikiwa. Tunataka Zanzibar ijuulikanayo duniani kupitia bidhaa tunazozilisha na mwani unaweza kutubeba kwa asilimia kubwa," aliongeza.

Hata hivyo, alikiri kuwepo changamoto zinazowakabili wajasiriamali katika kufikia masoko ya kimataifa ikiwemo ubora wa bidhaa wanazozizalisha.

Mapema, Meneja Mkuu wa DHL Tanzania, Paul Makalosi, alisema kampuni hiyo ina uzoefu wa kutosha wa usafirishaji wa mizigo na vifurushi duniani, hivyo ni fursa kwa wajasiriamali kuitumia. Aidha, alielezea, azma ya kampuni hiyo ya kuwafikia wajasiriamali katika utoaji wa huduma bora zitakazokidhi mahitaji ya soko la kimataifa la uuzaji na ununuzi.

“Kampuni yetu inayo uwezo mkubwa wa kusafirisha mizigo na bidhaa mbali mbali zaidi ya nchi 220 duniani kote,” amesema na kuongeza:

“Serikali ipo katika juhudi za kuwawezesha wajasiriamali kuingia kwenye biashara za kimataifa zaidi kwa njia ya mtandao ili waweze kupata wateja”.

Chanzo: --