Dar es Salaam. Mrembo wa dunia mwenye taji la uandishi wa habari (Miss Journalism World) Nina Yevtushenko ameahidi kuwa balozi mwaminifu wa vivutio vya utalii vilivyopo Tanzania na kuitangaza vyema nchi hiyo popote atakapokwenda duniani.
Yevtushenko ameyasema hayo jana Jumatatu Juni 3, 2019 baada ya kumaliza ziara yake ya kitalii iliyodumu nchini kwa muda wa wiki mbili.
Mrembo huyo kutoka nchi ya Ukraine alisema katika kipindi hicho amepata fursa ya kutembelea mbuga za Ngorongoro na Serengeti na kuona utajiri mkubwa ambao nchi ya Tanzania inao na unapaswa kutangazwa.
“Nilipofika Serengeti nilishangaa, ni kama nilikuwa kwenye nchi nyingine, Tanzania imebarikiwa na mimi nitakuwa balozi mzuri wa kuzungumza sifa hizi popote nitakapokwenda duniani, tayari kuna watu wameshaanza kuniuliza baada ya kuona picha zangu mtandaoni.”
“Nilienda pia Zanzibar nako nimeona vitu vizuri kwa kifupi naweza kusema Tanzania ni nchi nzuri na nitarudi tena kwanza heshima ya kukaribishwa bungeni Dodoma imenifanya nijione nina deni kwa ajili ya nchi hii, nimejipanga kusaidiana na watu wangu kuelezea vivutio vilivyopo hapa,” alisema Yevtushenko
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mwendeshaji wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) Devotha Mdachi alieleza ziara ya mrembo huyo inatarajiwa kuwa mwanzo wa kuingia soko la utalii la Ukraine na Urusi.
Pia Soma
- Morogoro yapangua safu ya sekta ya afya, nane wawekwa kando
- TPSF, Trademark East Africa wajazwa mamilioni ya kufadhili mikutano
- Naibu Waziri Mgumba ataka vijiji vitenge ardhi kuajiri vijana