Dodoma. Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Innocent Bashungwa amesema Serikali inakamilisha mkakati wa kuanzisha soko la chai nchini.
Amesema kwa kuanza, utaanza mnada wa kimataifa za zao hilo jijini Dar es Salaam.
Bashungwa ameyasema hayo leo Jumanne Septemba 3, 2019 wakati akijibu swali la mbunge wa Busekelo (CCM), Fred Mwakibete aliyehoji lini Serikali itatafuta soko la uhakika la zao hilo ambalo litasababisha kupanda kwa bei kuliko ya sasa ya Sh315 kwa kilo.
Akijibu swali hilo, Bashungwa amesema juhudi za Serikali kutafuta masoko ya mazao ya kilimo nchini ni endelevu.
Amesema jitihada zinazofanyika kwa zao hilo ni kuhakikisha kuwa chai inayozalishwa inauzwa nchini bila kuwalazimu wakulima kuisafirisha kwenda katika mnada mjini Mombasa.
Amesema katika kutekeleza uanzishwaji wa mnada tayari kikosi kazi kimeundwa kikijumuisha wadau mbalimbali wakiwemo Bodi ya Chai Tanzania (TBT), Soko la Bidhaa Tanzania (TMX), Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) na Chama cha wakulima wa Chai nchini (TAT).
Pia Soma
- Mahakama ya Tanzania ilivyomtumia salamu za tahadhari mrithi wa Tundu Lissu
- Huduma ya mionzi hospitali ya Haydom kuinufaisha mikoa sita