Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mlima Meru yazindua utalii wa baiskeli

Utalii Baiskeli.jpeg Baadhi ya watalii

Mon, 9 May 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania TANAPA, kwa kushirikiana na Kampuni ya Dorobo safari leo imezindua zao jipya la utalii la kupanda Mlima Meru kwa kutumia baiskeli ambapo zaidi ya watalii 20 wanapanda mlima huo ambao ni wa pili kwa urefu nchini Tanzania.

Akizindua zao hilo katika Hifadhi ya Taifa Arusha, Kamishna msaidizi wa Uhifadhi Albert Mziray ambaye ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Arusha amesema watalii hawa watatumia baiskeli kupanda mpaka kilele cha mlima Meru umbali wa mita 4566 juu ya usawa wa bahari

“Zao hili linakwenda kuungana na mazao mengine ya utalii yaliyopo katika Hifadhi hii ya Taifa Arusha, na matarajio yetu ni kuendelea kupata wageni wengi ili kuongeza pato la taifa na kuchangia katika kuendeleza shughuli za uhifadhi na utalii” alisema Kamishna Mziray.

Kwa upande wake Thad Peterson ambaye ni mkurugenzi wa Kampuni ya Utalii ya Dorobo Safari inayoshirikiana na Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) katika kufanikisha zoezi hili ameipongeza TANAPA kwa jitihada za kubuni mazao mapya ya utalii ili kuvutia zaidi watalii wa ndani na nje ya nchi kutembelea vivutio vya nchi yetu.

Akizungumza katika hafla hiyo ya uzinduzi katika Hifadhi ya Taifa Arusha Afisa Uhifadhi Mwandamizi Catherine Mbena anayeshughulikia Mawasiliano amebainisha

“ Tunazingatia mazingira husika na bidhaa zinazoweza kufanyika katika mazingira hayo

Shughuli ya kupanda mlima kwa baiskeli ipo katika Hifadhi ya Taifa Mlima Kilimanjaro na na leo tumezindua katika Hifadhi ya Taifa Arusha

Jukumu letu sisi ni kuhakikisha kila mtalii anaekuja kutembelea Hifadhi za Taifa anaridhika na huduma zetu, na tumejipanga kuhakikisha tunatimiza adhma ya serikali ya kufikisha watalii millioni 5 ifikapo mwaka 2025 kwa kuendelea kuwa wabunifu.”

Naye Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi Dkt. Bakari Mnaya anayesimamia shughuli za Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara katika kanda ya Kaskazini amebainisha uwepo wa mlima Meru, Misitu, na mandhari nzuri katika Hifadhi hii ya Arusha kuwa kichocheo cha aina hii ya utalii wa kuendesha Baiskeli kupanda Mlima.

Aidha, Kamishna Mnaya ametoa rai kwa wageni wa ndani na nje ya nchi kujitokeza kwa wingi kufanya aina hii ya utalii ambayo leo imezinduliwa katika hifadhi ya Taifa Arusha kwani ina faida lukuki kiafya.

“Pamoja kwamba ni burudani lakini pia ni njia ya kujenga mwili, kufanya mazoezi na kuweka afya vizuri alisema Kamishna Mnaya.”

Utalii wa kuendesha baiskeli umekuwa ukifanyika Hifadhi ya Taifa Arusha katika uwanda wa chini, na sasa umeongezwa utalii wa kupanda mlima kwa baiskeli.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live