Dar es Salaam. Kituo cha Uwekezaji Tanzania(TIC), kimetoa ufafanuzi wa hali ya uwekezaji nchini na kukanusha taarifa zinatolewa kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Akizungumza jana Alhamisi Juni 27, 2019 Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa TIC, Geoffrey Mwambe amesema baadhi ya miradi mikubwa ya uwekezaji inayoonekana kusimama, bado mazungumzo yanaendelea baina ya Serikali na wawekezaji.
Amesema mradi wa Liganga Mchuchuma, ni mradi mkubwa wa uwekezaji katika sekta ya nishati, unahusisha mradi wa kuchimba na kufua umeme unaotokana na makaa ya mawe utakaokwenda kuzalisha umeme 600MW.
“Miradi hii miwili inatekelezwa na Kampuni ya Tanzania China International Mineral resources limited, iliyoingia ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lenye asilimia 20 na kampuni ya Sichuan Hongda kutoka China yenye asilimia 80,” amesema mkurugenzi huyo.
Katika mradi wa usindikaji gesi wa NLG unaotarajiwa kujengwa mkoani Lindi, Mwambe amesema wawekezaji katika mradi huo ni Kampuni ya Equinor wenye asilimia 65 na mwekezaji mwingine ni ExxorMobil mwenye asilimia 35.
“Mradi huu bado uko katika mchakato wa majadiliano wa utekelezaji baina ya wawekezaji na Shirika la Taifa la Maendeleo la Petroli (TPDC), chini ya usimamizi wa Wizara ya Nishati,” amesema Mwambe.
Pia Soma
- Waziri wa Kenya azungumzia kauli ya Jaguar ndani ya Bunge la EALA
- Mfanyabiashara apambana na majambazi kwa dakika 15 na kuwanyang'anya bunduki aina ya Shotgun
- Polisi kuimarisha ulinzi maonyesho ya Sabasaba