Wafanya kazi wa Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania wamemuanga Mkurungenzi wao anayeondoka baada ya kuhudumu kwenye kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka sita.
Akiongea kwenye hafla hiyo, Mkurungenzi huyo anayeondoka Bw, Sunil Colaso alisema kuwa Tanzania imekuwa ni kama nyumbani na hatua hii ya kuwaaga ni ngumu baada ya kuishi na kufanya kazi kwa miaka sita Tanzania.
“Nachukua fursa hii kuwashukuru wafanya kazi wote wa Airtel kwa muda wote tuliofanya kazi pamoja. Tumeshirikiana kufanya kazi kwa bidii na umoja wenu ulifanya kazi yangu kuwa rahisi na kufanikisha malengo yetu. Ni imani yangu kuwa leo wakati naondoka ninaacha nyuma timu imara ambayo itaendelea kuwatumikia Watanzania kwa huduma bora za mawasiliano kila siku,” alisema Colaso.
Alitoa wito kwa wafanya kazi na wadau wengine kumuunga mkono Mkurugenzi mpya George Mathen anayetarajiwa hapa nchini kuanzia kesho Oktoba 1, ili kupata mafanikio makubwa zaidi ya aliopata.
Colaso pia akitoa shukrani kwa Serikali ya Tanzania, Wizara na Taasisi zake zote kwa kuiunga mkono Airtel Tanzania kwa kipindi chote cha uongozi wake.
“Nashukuru kwa dhati serikali kwa kutuunga mkono Airtel Tanzania, ndio maana tumefanikiwa kutoa huduma bora kimataifa na hapa nchini hasa kwenye huduma za Airtel Money, Airtel yatosha bando inayowafaidisha wateja kwa huduma za kupiga simu pamoja na intaneti. Nawapongeza pia wafanyakazi wote wa Airtel kwa kuwa na mafanikio ya kipekee ya kuweza kusambaza huduma za Airtel Money mpaka vijijin ambapo hadi sasa mmefungua zaidi ya maduka ya Airtel Money 900,”alisema Colaso
Pia Soma
- Watoto wa miaka minne Ghana kufundishwa elimu ya uzazi
- Trump ataka kukutana na mtu aliyetoa siri dhidi yake
- Matumizi ya noti ya Sh1,000 mwisho leo Kenya
“Tunamuaga leo Mkurugenzi Sunil Colaso, alikuwa ni mtu wa kupenda kazi yake, kujitolea kusaidiana na wafanyakazi kila alipohitajika, alipenda kufanya kazi kwa umoja, haya ni kati ya mambo ambayo tutamkumbuka nayo. Alikuwa ni mtu mwenye sifa zote za kiongozi na mwenye kujenga timu ya pamoja, alimpa kila mfanyakazi wa Airtel Tanzania nafasi ya kuonyesha uwezo wake.’ Singano alieleza.