Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Uwekezaji, Prof Kitila Mkumbo amewataka watanzania kuacha fikra kuwa suala la uwekezaji linahitaji watu kutoka nje ya nchi pekee na kusisitiza ni lazima kuwe na uthubutu katika kuwekeza hata kwa mtaji mdogo na hatimaye kupata faida.
Akizungumza muda mfupi uliopita katika hafla ya Uzinduzi wa Kitabu cha Fursa za Uwekezaji Katika mkoani Katavi, Prof Mkumbo amewataka wakazi wa mkoa huo kuacha uoga katika kufanya uwekezaji na badala yake wathubutu kwa manufaa ya Taifa.
“Wakati mwingine tukizungumzia uwekezaji watu wengi wanaona kama jambo kubwa hivi, zito na linahitaji wageni lakini sio hivyo uwekezaji ni hatua yoyote mtu anayochukua yeye binfsi au kampuni kuweka mtaji wa kufanya biashara na hatimaye kupata faida” amesema Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Uwekezaji, Prof Kitila Mkumbo.
Aidha, Prof Mkumbo amebainisha kuwa siku zote uchumi na fedha duniani hutegemea uwepo wa watu wanaofanya kazi kwa bidii na maarifa ambao wako tayari kuweka akiba pamoja na kuwekeza.
“Uchumi wa leo unategemea sana hilo lazima wawepo watu wa kuweka akiba lakini pia kuwekeza wakichagizwa na kufanya kazi kwa bidii na maarifa hili jambo ni muhimu duniani kote kwenye ukuaji wa uchumi” amesema Prof Mkumbo.