Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imepiga marufuku uuzwaji holela wa makasha yanayotumika kubeba, kusambaza na kuhifadhia kemikali hatarishi kwa mazingira huku ikitahadharisha watakaokiuka marufuku hiyo kuwa watakumbana faini kati ya Sh5 milioni hadi Sh200 milioni ama kifungo.
Marufuku hiyo imetangazwa jana Jumatatu Novemba 13, 2023, na Mkurugenzi wa Huduma za Udhibiti, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali, Daniel Ndiyo ambapo amesema wamefikia uamuzi huo baada ya kubaini kuna wafanyabiashara wanaouza makasha hayo kiholela bila kujua athari zake.
Akitolea mfano Mtaa wa darajani eneo la Natta jijini Mwanza, Ndiyo amesema maabara ya mkemia mkuu, Kanda ya Ziwa ilibaini uuzwaji holela wa makasha yaliyotumika kuhifadhi ama kusambazia kemikali, ndipo elimu ya matumizi sahihi ya makasha hayo ilipotolewa ili kuongeza uelewa, kupunguza madhara kwa jamii.