Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Kampuni ya Mkaa Endelevu inayozalisha mkaa kwa kutumia pumba za mbao, Benjamin lane amesema kama njia za panya zinazotumika kuingiza mkaa kwenye miji na majiji zikizuiwa na wafanyabiashara kuanza kutozwa kodi mazingira yatasalimika.
Land amesema bei ya mkaa ikiongezeka watumiaji watatafuta njia nyingine ya nishati tofauti na sasa ambapo mkaa mwingi unaingizwa kinyemela.
Akizungumzia mada ya 'Tutafute Suluhisho Pamoja' kupitia Mwananchi Jukwaa la Fikra linaloendeshwa kwa ushirikiano na ITV na Radio One, katika ukumbi wa Kisenga, jijini Dar es Salaam, Land amesema inawezekana kuhifadhi mazingira kwa kuacha kukata miti.
Amesema zipo njia nyingi zinaweza kutumika kuzalisha mkaa na si kutegemea miti peke yake.
"Kuna wakati unaweza ona mkaa unaoingia ni kidogo lakini unaweza jaa kwenye magari makubwa ya semitrela kati ya manne hadi matano kwa wiki, ni mwingi sana," amesema.
Land amesema kwa sasa kampuni yao inazalisha mkaa huo kwa kutegemea pumba kutoka Mafinga, Mufindi mkoani Iringa.