Arusha. Mjasiriamali Marijani Mmari anayefanya biashara ya ufugaji kuku eneo la Makumira wilayani Arumeru, ameshinda tuzo ya mjasiriamali bora inayotolewa na Citi Bank.
Akizungumza na waandishi wa habari katika eneo lake la ufugaji leo Jumatano Oktoba 2, 2019, Mmari alisema ameshinda tuzo hiyo, kutokana na kupanua biashara yake baada ya kupatiwa mkpo na taasisi ya Brac.
Amesema alianza ufugaji mwaka 2011 akiwa na kuku 200 lakini aliweza kupata mkopo kutoka Brac wa Sh4 milioni hadi Sh13 milioni ambao sasa umewezesha kuongeza kuku na kufuga kisasa.
“Hivi sasa biashara yangu ni nzuri, nimetoa ajira kwa vijana 15, nimenunua gari nasomesha watoto na nina maduka mawili kutokana na kazi hii ya ufugaji,” amesema.
Amesema anaishukuru Brac kwa kumsaidia hata kushinda tuzo ya Citi Bank ambao walimzawadia kiasi cha Dola 1,000 za Marekani ili kupanua zaidi biashara yake.
Ofisa mikopo wa Brac eneo la Usa River, Mary Richard amesema ushindi wa Mmari ni faraja kwao kwa sababu tangu mwaka 2015 alikuwa mteja mzuri na amekuwa na mafanikio makubwa.
Pia Soma
- Naibu waziri Kandege atoa mwanga watumiaji mabasi yaendayo haraka Dar
- Mfanyabiashara akiri makosa, ahukumiwa kulipa Sh100 milioni
- Exim yazindua akaunti tatu mpya
Mmari ni mteja wa tatu kutoka Brac kushinda tuzo hiyo wengine waliowahi kutunukiwa tuzo hiyo ni Zabron Mbwaga pia kutoka mkoa wa Arusha na Lucy Kiongosi kutoka Dodoma.