Mfumuko wa bei nchini Marekani ulifikia kilele kipya cha asilimia 9.1 mwezi Juni, na kuziweka katika hali ngumu familia za Wamarekani na kuongeza shinikizo kwa Rais Joe Biden, ambaye viwango vya utendaji kazi wake vinazidi kuporomoka kutokana na kupanda kwa bei kusikokoma.
Takwimu ambazo zilitolewa na serikali Jumatano zimeonyesha ongezeko kubwa la bei za bidhaa ambalo halikutarajiwa ikilinganishwa na mwezi Mei, ongezeko hilo likichochewa na bei ya juu ya petroli.
Mfumko huo wa asilimia 9.1 katika kipindi cha miezi 12 iliyopita hadi Juni ulikuwa mfumko mkubwa na wa haraka tangu Novemba 1981, wizara ya kazi imeripoti.
Nishati ilichangia kwa asilimia 50 kwenye ongezeko hilo la kila mwezi, huku bei ya petroli ikiongezeka kwa asilimia 11.2 mwezi uliopita, na kufikia kiwango cha asilimia 59.9 katika mwaka uliopita. Bei ya jumla ya nishati ilifikia ongezeko kubwa la kila mwaka tangu Aprili 1980.