MCHIMBAJI mdogo wa madini aina ya Tanzanite, Saninniu Laizer, leo ametambulika na Wizara ya Madini kuwa ni mmoja kati ya watu mabilionea baada ya kupata mawe makubwa mawili yenye thamani ya Shilingi Bilioni 7.8.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila, baada ya kukagua mawe hayo, huku akitoa ufafanuzi wa mawe hayo kwamba jiwe moja lina kilo 9.2 ambalo thamani yake ni Shilingi Bilioni 4.5 na jiwe la pili lina kilo 5.8 lenye thamani ya Shilingi Bilioni 3.3.
Profesa Msanjila amesema mawe hayo ni tofauti na mawe mengine ambayo yameshawahi kupatikana katika machimbo ta Tanzanite.
“Na utofauti wake ni kwamba mawe ya uzito huo hayajawahi kupatikana kwenye machimbo ya tanzanite tangu machimbo yaanze na yamepatikana ndani ya ukuta wa Mirereni kwahiyo hii ni rekodi mpya ya kupata mawe yenye uzito huo” amesema Prof. Msanjila
Aidha, Profesa Msanjila amesema Sekta ya Madini inauwezo wa kumfanya mtu kuwa Bilionea kwa haraka, lakini pia amewasihi wananchi kuwekeza kwa dhati katika sekta hiyo.