Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mchimba madini atoa milioni 120/- kuhamisha shule

Bb53fda8ed7ba2c361c5f51eef104baf Mchimba madini atoa milioni 120/- kuhamisha shule

Fri, 29 Jan 2021 Chanzo: habarileo.co.tz

MCHIMBAJI mdogo wa madini ya dhahabu katika kijiji cha Kakumbi, kata ya Lugunga, wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita, Ngabanya Gilu ametoa Sh milioni 120 na kuhamisha Shule ya Sekondari Kakumbi.

Mchimbaji huyo alisema hayo baada ya kumkabidhi Diwani Kata ya Lugunga, Enock John mifuko 600 ya saruji kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa miundombinu ya shule mpya ya sekondari iliyohamishwa.

Gilu alihamisha shule hiyo na kutafuta eneo jingine kwa ajili ya kupisha kuchimba madini ya dhahabu.

Ujenzi wa shule mpya ya sekondari Kakumbi umeanza baada ya makubaliano baina ya mchimbaji huyo madini na wananchi.

"Nimetoa Sh milioni 120 kwa ajili ya kuanza kujengwa upya Shule ya Sekondari Kakumbi kwa makubaliano na wananchi wa eneo hilo na itaanza na ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa, matundu ya vyoo sita pamoja jengo la utawala na nyumba mbili za walimu, nitaendelea kuwasaidia pale ambapo msaada zaidi utahitajika," alisema Gilu.

Kwa upande wake Diwani wa kata hiyo, John alisema shule mpya ya sekondari inayojengwa katika kijiji cha Kakumbi ni ya pili kwenye kata hiyo.

Alisema kujengwa kwa shule hiyo kutasaidia kupunguza mwendo mrefu wanaotembea wanafunzi kufuata masomo Shule ya Sekondari Masumbwe na Lugunga.

Alisema mchimbaji madini huyo amefanya hivyo kutokana na makubaliano na serikali ya kata kwamba ahamishe miundombinu ya shule kwenda katika kijiji hicho na kujenga vyumba viwili vya madarasa, nyumba mbili za walimu na matundu sita ya vyoo vya wanafunzi na walimu ili kumpisha aweze kuendesha shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu.

"Mchimbaji baada ya kuvutiwa na eneo hilo akalipa tena upya wananchi hao na kutimiza Sh milioni 120 pamoja na ujenzi wa miundombinu ya vyumba vya madarasa, lakini pia tulimuomba mifuko ya saruji ili tufyatuwe matofali wenyewe pamoja na kujenga, jambo ambalo tulifanikiwa," alisema diwani huyo.

John alisema kipindi cha mwaka 2006 wananchi walianzisha ujenzi wa shule ya sekondari kwenye eneo la Mashariki kwa lengo la kupunguza mwendo mrefu wanaotembea watoto kufuata masomo baada ya kuibuka madini ya dhahabu kwenye eneo hilo, Ngabanya alikubaliana na wananchi kuhamisha shule hiyo.

Mratibu Elimu Kata ya Lugunga, Jacob Komba alikiri mchimbaji huyo kutumia Sh milioni 120 kulipa fidia kwa wamiliki wa maeneo hayo na kufaanya ujenzi wa vyumba vya madarasa vya shule hiyo mpya ya sekondari.

Chanzo: habarileo.co.tz