Dar es Salaam. Mchakato wa kutafuta kampuni 100 bora za kiwango cha kati umezinduliwa leo Alhamisi Oktoba 24, 2019 huku asilimia 66 ya washiriki wakiwa wazawa.
Uzinduzi huo umefanyika leo ambako waandaaji ambao ni kampuni ya Hesabu ya KPMG na kampuni ya Mwananchi Communication’s Ltd (MCL) wameungana na wadhamini wengine wa shindano hilo.
Akizungumza katika uzinduzi huo mtafiti, Dk Remidius Ruhinduka amesema asilimia 34 ya kampuni zilizoshiriki zinamilikiwa kwa ubia baina ya wageni na wazawa, nyingine zinamilikiwa na wazawa.
Alexander Njombe wa KPMG amesema kampuni zinazoingia kwenye shindano hilo ni zenye mauzo yanayoanzia Sh1 bilioni mpaka Sh20 bilioni, “tunaangalia kumbukumbu zake za fedha kwa miaka mitatu iliyopita.”
Wadhamini wengine wa shindano hilo ni Benki ya CRDB, Azam TV, FSDT na hoteli ya Serena.