Dar es Salaam. Mbunge wa Jimbo la Mbagala, Issa Mangungu amesema majukwaa ya wanawake yasiishie kwenye uzinduzi pekee bali yalenge kuhakikisha wanawake wanajikwamua kiuchumi.
Mangungu aliyasema hayo wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Wanawake Mtaa wa Kiponza, Mbande wilayani Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam jana Jumamosi.
Alisema nia ya Serikali ni kuona wanawake wanajikwamua , hivyo wanatakiwa kubuni miradi na kuiendeleza, ambapo serikali pia itashirikiana nao ili kufikia uchumi wa viwanda.
Naye, Diwani wa Kata ya Chamazi, Hemed Karata aliwapongeza wanawake wa Mtaa wa Kiponza kufanikisha uzinduzi wa jukwaa hilo. Aliongeza kuwai huo ndio ulikuwa mtaa wa mwisho kati ya mtaa tisa ya Kata ya Chamazi, Hivyo aliwataka wanawake hao kujiendeleza kupitia jukwaa hilo lililozinduliwa.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wanawake, Stukia Ally alisema lengo la kuanzisha jukwaa hilo ni kuwaweka wanawake karibu ili kuwa na umoja ambao utawasaidia katika uzalishaji.
Alisema wanawake hao wanapaswa kuitumia vyema fursa hiyo ili waweze kujiletea maendeleo.
“Ili tufikie maendeleo lazima tuwe na moyo wa kujitilea, kupendana na kuwa na wivu wa maendeleo. Lengo ni kuweza kujiendeleza kisha kujiinua kiuchumi katika jamii,” alisema Stukia.