Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mazao ya biashara kuuzwa kupitia ushirika

6860 MAJALIWA K TZW

Sun, 22 Apr 2018 Chanzo: habarileo.co.tz

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema katika msimu huu wa kilimo, mazao yote ya biashara yatauzwa kupitia vyama vya ushirika vilivyopo. Alitoa kauli hiyo jana mjini hapa katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi katika Mradi wa Ujenzi wa Vihenge na Maghala ya Kisasa ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), ambao utafanyika katika kanda nane za wakala.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema kwa sasa serikali imejipanga katika msimu huu wa kilimo mazao yote ya biashara kuuzwa kupitia vyama vya ushirika. Kutokana na hilo, amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya kuhakikisha vyama hivyo vinakuwa na viongozi waadilifu na waaminifu.

“Wakuu wa mikoa hakikisheni vyama vya ushirika vinakuwa na watu makini, simamieni ushirika ili uwanufaishe wananchi," alisema na kuongeza kuwa hatua ya kuuza mazao kupitia vyama vya ushirika itasaidia wakulima kutolaliwa na wafanyabiashara pindi watakapotaka kununua kwa bei ndogo.

Aidha, ameitaka jamii kujenga utamaduni wa kuhifadhi chakula katika ngazi ya kaya. Alisema serikali imedhamiria kwa dhati kuongeza uwezo wa uhifadhi wa chakula kuweza kufikia tani laki 700,000 ifikapo mwaka 2025. Pia aliwataka wananchi kutumia fursa ya mvua zinazonyesha kulima mazao mengi.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mahmoud Mgimwa aliitaka serikali kuiangalia kipekee Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA).

Mgimwa alisema kama serikali haitaongeza fedha, maghala na vihenge vinavyojengwa havitakuwa na tija. Alisema ujenzi huo utakuwa na tija kama fedha zilizoombwa na NFRA katika bajeti yake zitatolewa.

Mwenyekiti huyo alisema katika mwaka wa fedha 2018/19, Wakala huo umeomba kiasi cha Sh bilioni 86 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yake ikiwemo kununua mazao ya wakulima.

Waziri wa Kilimo, Dk Charles Tizeba alisema changamoto wanazokutana nazo ni pamoja na katika msimu wa mvua waliingia panya na wadudu aina ya viwavijeshi ambao alidai wamekuwa wakila mazao ya wakulima.

Alisema wamejipanga kukabiliana nao kwa kuwataka wakurugenzi kutoa taarifa pindi wanapoona panya hao kwa wizara yake ili dawa ya kuwazuia itumwe.

Kaimu Mtendaji wa NFRA, Vumilia Zikankuba alisema mradi huo utatekelezwa katika maeneo nane ya wakala ambayo ni Songea, Makambako, Mbozi, Sumbawanga, Mpanda, Shinyanga, Dodoma na Babati. Zikankuba alisema NFRA inamiliki maghala ya kuhifadhi nafaka 34 yenye uwezo wa kuhifadhi tani 251,000.

Alisema uwezo huo wa sasa hautoshelezi mahitaji ya dharura ya chakula kwa mfululizo wa miezi mitatu kwa akiba isiyopungua tani 700,000, hivyo kuwapo uhitaji wa kuongeza uwezo wa kuhifadhi.

Chanzo: habarileo.co.tz