Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mawakala wa Bima wapewa darasa

Mafunzo Pic Mawakala wa Bima wapewa darasa

Tue, 4 Apr 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa kushirikiana na Kampuni ya Bima ya Britam Tanzania wamezindua mafunzo maalum kwa mawakala wa benki hiyo mikoa ya Kanda ya Ziwa na Kanda ya Kaskazini yanayolenga kuwajengea uwezo mawakala hao ili waweze kutoa huduma za Bima.

Mafunzo hayo ya wiki moja yanaendelea katika mikoa ya Mwanza na Arusha yakiendeshwa kupitia Chuo cha Usimamizi wa Bima na Hifadhi ya Jamii Afrika (ACISP).

Wakizungumzia hatua hiyo Mkurugenzi wa Wateja binafsi wa Benki ya NBC, Elibariki Masuke pamoja na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Bima ya Britam Tanzania, Raymond Komanga walisema mafunzo hayo yanalenga kupanua wigo wa utoaji wa huduma za bima nchini kutokana na ukubwa wa mtandao wa makala wa benki hiyo kote nchini.

“Kupitia mafunzo haya tunakwenda kuongeza wigo wa watoa huduma za Bima nchini hasa kwa kuzingatia kwamba NBC tayari tuna mtandao wa mawakala 10,000 kote nchini ambao kupitia mafunzo haya watajengewa uwezo na kupatiwa vigezo vitakavyo wawezesha kutoa huduma za Bima pia.’’

“Ni fursa kwa mawakala wetu kuongeza kipato kwa kuwa sasa hawatafanya tu miamala ya kibenki bali pia wataanza kufanya miamala ya kibima na na hivyo kujiongezea kipato kupitia ‘kamisheni’,’’ alisema Masuke.

Kwa mujibu wa Masuke hatua hiyo ni muendelezo wa mkakati wa benki hiyo katika kusogeza zaidi huduma zake karibu na wananchi ikiwa ni muitikio wa wito wa serikali unaohamasisha taasisi za fedha nchini kusogeza zaidi huduma zao ili ziweze kuwafikia wananchi wengi zaidi.

“Kama ambavyo tumeweza kusogeza huduma zetu za kibenki kupitia mawakala hawa lengo letu pia ni kuona huduma za kibima tunazozitoa kwa kushirikiana na kampuni mbalimbali za Bima ikiwemo Britam Tanzania zinaweza kuwafikia wananchi kwa ukaribu zaidi pia,’’ aliongeza.

Kwa upande wake Komanga alisema mafunzo hayo yanayodhaminiwa na kampuni hiyo yamekuja kufuatia muitikio mzuri wa soko la huduma za Bima hapa nchini licha ya uhaba wa mawakala na madalali wa bima nchini.

“Licha uhaba huo, mwaka jana soko la Bima liliweza kukusanya ada za Bima (Premiums) kiasi cha Sh1.1 Trilioni kupitia mawakala na madalali wa Bima waliopo sasa. Kufuatia mafanikio haya tukaona ni wakati muafaka sasa kupanua wigo zaidi wa kuwafikia wateja wetu nchi nzima kupitia mawakala wa wenzetu Benki ya NBC waliopo nchi nzima. Kupitia mafunzo haya tunatarajia matokeo mazuri zaidi kwa kuwa idadi ya mawakala wa bima inaenda kuwa kubwa zaidi,’’ alisema.

Kwa mujibu wa Komanga mafunzo hayo ya wiki moja kwa Kanda ya Ziwa yatahusisha mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Geita, Simiyu, Mara na Kagera huku katika mikoa ya Kanda ya Kaskazini yakihusisha mikoa ya Arusha na Kilimanjaro.

Akizungumzia mafunzo hayo Mwenyekiti Mtendaji Chuo cha Usimamizi wa Bima na Hifadhi ya Jamii cha Africa Bw Sosthenes Kewe alisema yanalenga kuwawezesha mawakala hao waweze kupata vigezo vya awali vitakavyowawezesha kutoa huduma za Bima kulingana na vigezo vilivyowekwa na Mamlaka ya Bima Tanzania (TIRA).

“Tunatarajia kwamba baada ya mafunzo haya washiriki wote watapata nafasi ya kufanya mitihani ya kuhitimu na vyeti vitatolewa kwa wale tu watakaofaulu mitihani hiyo,’’ alinainisha.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live