Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Mauzo maharage ya Tanzania EAC yafikia Dola milioni 193

001e7d5f3798f4037d7e0a3be817d26d Mauzo maharage ya Tanzania EAC yafikia Dola milioni 193

Tue, 24 May 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mauzo ya maharage kutoka Tanzania katika nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) yamefikia Dola za Marekani milioni 193.

Kuongezeka kwa mauzo hayo kunatokana na juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan kuimarisha uhusiano na mataifa wanachama wa EAC na mataifa mengine.

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe alibainisha hayo bungeni Dodoma wakati akisoma hotuba ya bajeti ya wizara hiyo ya mwaka wa fedha 2022/2023.

Alisema mwaka 2020 mahitaji ya maharage nchini yalikuwa tani milioni moja, lakini uzalishaji ulivuka lengo na kufikia tani milioni 1.2 kutokana na mipango mbalimbali iliyowekwa ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

Kwa mujibu wa Bashe, kuongezeka kwa mauzo ya maharage kumechangiwa na kuondolewa kwa vikwazo 56 vya biashara kati ya 64 vilivyokuwapo kati ya Tanzania na Kenya.

Alisema juhudi hizo zimesababisha ukuaji wa biashara kati ya Tanzania na Kenya kufikia Dola za Marekani milioni 905, pamoja na upatikanaji wa soko la China kwa ajili ya maharage ya soya na mihogo, jambo ambalo limetoa fursa ya soko la uhakika kwa wakulima wa mazao hayo nchini.

Hivi karibuni, mratibu wa zao la maharage kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (Tari) Kituo cha Ilonga, mkoani Mbeya, Dk Rose Mongi alisema Tanzania inaongoza kwa kilimo cha maharage katika EAC.

Hata hivyo, alisema licha ya kuongoza bado mahitaji ni makubwa kwani hivi sasa mazao yanayozalishwa nchini yanauzwa katika nchi za Zambia, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Malawi, Rwanda na Burundi.

Alisema kutokana na mahitaji kuwa makubwa, Tanzania ina fursa ya kuongeza uzalishaji, hivyo Kituo cha Uyole kinafanya utafiti wa zao hilo ili Watanzania wapate mbegu bora itakayowawezesha kujikimu na kupata ziada ya kuuza.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live