Dar es salaam. Kongamano la Kimataifa la Mafuta na Gesi nchini Tanzania kwa mara ya tatu mfululizo litahusisha maeneo mapya matano ikiwamo tuzo tatu kwa kampuni bora zinazofanya vyema kwenye sekta hiyo.
Kauli hiyo imetolewa leo Septemba 30, 2019 na Mratibu wa kongamano hilo, Abdulsamad Abdulrahim alipokuwa akizungumza na wanahabari jijini Dar es salaam.
Kongamano hilo limeandaliwa Kwa ushirikiano wa Jumuiya ya Watoa huduma ya Mafuta na Gesi nchini (Atogs), Ewura, PURA, TPDC, pamoja na Kampuni inayoandaa makongamano ya Kimataifa(CWC Group).
"Lakini pia Kongamano hilo tutatoa kipaumbele cha kuwatambua wanawake champions wanaofanya vizuri katika sekta ili kuhamasisha wanawake wengi zaidi kuingia kwenye fursa za sekta hii," amesema Abdulsamad.
Mambo mengine mapya ni pamoja na kuwa na uwakilishi wa mjasiriamali kutoka mikoa yote nchini, matumizi ya teknolojia ya mawasiliano wakati wa Kongamano pamoja na utoaji wa zawadi kwa washindi watatu wa uandishi wa Insha.
Pia Soma
- Watoto wa miaka minne Ghana kufundishwa elimu ya uzazi
- Trump ataka kukutana na mtu aliyetoa siri dhidi yake
- Mkurugenzi Airtel Tanzania aaga wafanyakazi, aishukuru Serikali
Kwa mwaka huu, kongamano hilo litakuwa na mijadala inayohusu matumizi ya teknolojia katika sekta na taarifa za mabadiliko ya biashara.
Ajenda nyingine ni kuangalia uhusiano katika fursa za sekta na mikakati ya Tanzania ya Viwanda, mbinu za kuingia ubia na Kampuni za Kimataifa na uwezeshaji wa Kampuni za ndani.
Makamu wa Rais wa Kampuni ya CWC ambao ni wawezeshaji wakubwa wa Kongamano hilo, Tiago Marques amesema Kongamano hilo ni mchango mkubwa kwa nchi kunufaika na rasilimali hiyo.
Miongoni mwa matokeo chanya ya makongamano yaliyopita ni pamoja na Kampuni kadhaa kuingia ubia au kuwekeza ndani.
Baadhi ya kampuni hizo ni AGS, IMI international na Worley ya Uingereza.