Baadhi ya mataifa nje ya Afrika yameomba kujiunga kama wanachama waangalizi katika Jumuiya ya Nchi Zinazozalisha Almasi Afrika (ADPA) zikiwemo taasisi zilizobobea kwenye masuala ya madini hayo.
Hayo yamebainishwa na Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko wakati akifunga Mkutano wa Tatu wa Dharurra wa Baraza la Mawaziri wa jumuiya hiyo uliofanyika jijini Arusha na kutanguliwa na mkutano wa wataalam kutoka mataifa wanachama.
Dkt.Biteko aliongeza kwamba, suala hilo lilikuwa miongoni mwa ajenda tatu zilizojadiliwa katika mkutano huo na kwamba jumuiya hiyo imepanga kuangalia sifa na vigezo kwa nchi hizo na wakati utakapowadia italazimika kubadilisha Katiba ya jumuiya hiyo.
Lengo likiwa ni kutoa fursa kwa nchi hizo kujiunga waweze kuendelea kujengeana uwezo na kubadilisha uzoefu na nchi zilizo nje ya Afrika katika masuala ya almasi.
Pia, alisema kuwa ajenda nyingine iliyojadiliwa katika kikao hicho ni kuhusu uteuzi wa watendaji wa kudumu katika sekretatieti ya umoja huo ambapo baraza liliamua hadi kufikia katikati ya mwezi Septemba, mwaka huu watendaji hao wawe wamepatikana.