Tarime. Ofisa madini wa Mkoa wa Mara nchini Tanzania, Nyaisara Mgaya amesema masoko matatu ya madini yatafunguliwa kabla ya kumalizika mwezi Agosti, 2019.
Amesema hatua hiyo itafanya masoko ya madini katika Mkoa huo kuwa manne.
Akitoa taarifa ya idara ya madini mkoani humo, Mgaya amesema masoko hayo matatu yatafunguliwa Wilaya za Tarime na Butiama baada ya kukamilika kwa maandalizi.
Amebainisha kuwa lengo ni kuboresha sekta ya madini ikiwemo ukusanyaji wa mapato yatokanayo na madini baada ya mafanikio yaliyopatikana kwa kufunguliwa kwa soko la kwanza la madini mjini Musoma.
Amesema tangu kufunguliwa kwa soko lililopo sasa katika mji wa Musoma, Serikali imepata Sh698.6 milioni ikiwemo ada ya ukaguzi na mrabaha baada ya zaidi ya gramu 114, 111 za madini kuuzwa katika soko hilo kuanzia Mei hadi Julai, 2019.