Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango amepiga marufuku ununuzi wa mazao ya wakulima kwa kutumia vipimo visivyokuwa rasmi ikiwemo ujazo ulizidi yaani lumbesa
Alitoa agizo hilo jana alipokuwa akizindua Maonesho ya Wakulima (Nanenane) ambayo kitaifa yanafanyika katika viwanja vya John Mwakangale jijini hapo.
Dk. Mpango alisema, kuanzia sasa mazao yote yanatakiwa kuuzwa kwa kupimwa kwenye mizani huku akiwataka wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya zote nchini kusimamia matumizi ya vipimo hivyo.
Alisema hata mifugo inatakiwa kuuzwa kwa kutumia mizani na kuagiza ielekezwe kwenye minada yote ya mazao ili itumike kupima mazao ya wakulima.
“Kuanzia sasa lumbesa nchini ‘no’ (hapana), kwa hiyo mazao yote yatanunuliwa kwa kutumia mizani, nawaagiza wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya msimamie hili, hatutaki kusikia mahali popote biashara hii ikiendelea,” alisema Dk. Mpango.
Alisema faini za lumbesa hazitatakiwa kuwa chanzo cha kuendelea kutumika kwa vipimo hivyo visivyostahili kwenye ununuzi wa mazao ya wakulima.