SERIKALI kupitia Wizara ya Kilimo itafanyia kazi marufuku ya kuuza miwa nje ya eneo la mwekezaji kwa kuwa hatua hiyo inadidimiza juhudi za serikali kukuza uzalishaji wa miwa huku ikimkandamiza mkulima kwa kumkosesha soko huku miwa ikiharibikia shambani.
Aidha, Waziri wa Kilimo, Profesa Adolf Mkenda, ametoa onyo kwa kuwataka wawekezaji wa viwanda vya sukari vya Kilombero na Mtibwa kuondoa zuio la wakulima kuuza miwa yao kwa watu wengine kwa kigezo cha kulinda soko la ndani kwa kuwa zuio hilo linasababisha upungufu wa sukari nchini.
Profesa Mkenda, alisema hayo juzi alipotembelea Kiwanda cha Mkulazi II na kuzungumza na wakulima wa miwa wa Bonde la Mbigiri kutoka vijiji vya Msowero, Malangali, Mvumi, Wami, Dakwa na Mbigiri wilayani Kilosa katika Mkoa wa Morogoro.
"Wizara itaangalia upya marufuku hii ya kuzuia wakulima kuuza miwa inayozipa nafuu kampuni za Kilombero na Mtibwa pekee kuwa wanunuzi pekee wa miwa ya wakulima na hivyo, kuwafanya wafanyabiashara wengine wenye nia ya kununua miwa kushindwa," alisema.
Alisema kuwapo kwa wanunuzi wengi wa miwa huleta nafuu kwa wakulima kuchagua nani wamuuzie miwa hali inayoongeza ushindani wa bei katika soko.