Dar es Salaam. Jengo la Taasisi ya Mwalimu Nyerere lililojengwa na Kampuni tanzu ya CRJE LTD, linazinduliwa rasmi kesho.
Uzinduzi huo utafanywa na Rais John Magufuli wa Tanzania na Yoweri Museven wa Uganda.
Marais hao ambao pia watashiriki mdahalo juu ya mtizamo na maono ya Hayati Mwalimu Julius Nyerere kuhusu maendeleo, umoja, amani, kujitegemea kiuchumi na viwanda hapa nchini, watafanya uzinduzi huo jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Alhamis Septemba 5, 2019, na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku, inasema Rais Magufuli na Museveni watakuwa wageni rasmi katika ufunguzi huo.
Jengo hilo lipo Barabara ya Morogoro eneo lijulikanalo kama 'MNF Square'.
Amesema litakuwa na ofisi za utawala, maktaba itakayokuwa na nyaraka na kumbukumbu za Baba wa Taifa zinazohusu maendeleo, amani, umoja na mfumo wa uchumi duniani na pia chuo cha mafunzo ya uongozi.
Pia Soma
- Wanusurika kifo basi likipinduka mkoani Simiyu
- Sita kortini kwa kusafirisha bangi kilo 197.49
- Wanawake kuwekewa mazingira wezeshi ya ufanyaji biashara mipakani
- Kesi ya wanafunzi wa KIU kumdhihaki Rais Magufuli kuendelea Oktoba 8
“Jengo hili pia lina eneo la takribani mita za mraba 3,600 ambazo zinapangishwa kwa ajili ya kuipatia taasisi mapato ya kujiendesha, litajumuisha hoteli ya kiwango cha nyota tano, ya kwanza nchini , ijulikanayo kama Johari Rotana na mwendeshaji wake ni Rotana Hotels corporation ya Dubai,” amesema Butiku.
Amesema jengo hilo linamilikiwa na taasisi ya Mwalimu Nyerere na limejengwa kwa mkopo wa CRJE ambayo ni kampuni tanzu ya CRJE LTD inayomilikiwa na shirika la umma la Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China na IFC.