Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Majaliwa: Ruksa kuuza mahindi nje ya Tanzania

Fri, 9 Nov 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dodoma. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema ni ruksa kwa wakulima kuuza mahindi nje ya nchi ilimradi watoe taarifa serikalini.

Katika majibu yake kwa maswali ya papo kwa hapo bungeni leo Alhamisi Novemba 8, 2018, Waziri Mkuu amesema pia Tanzania inaruhusu kuingiza mahindi ndani ya nchi ilimradi kuwepo na vibali maalumu kutoka katika mamlaka husika.

Katika swali lake, Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Lucy Mlowe ametaka kujua nini kauli ya Serikali kuhusu mahindi mengi ambayo yamekosa soko na kuwakosesha kipato wakulima ikiwemo mkoa wa Rukwa.

"Wakulima wanaruhusiwa kuuza mahindi nje ya nchi, jambo la muhimu hapa ni kuhakikisha kunakuwepo na taarifa sahihi ndani ya Serikali ili tuweze kujiridhisha kama nchi ina chakula cha kutosha," amesema Waziri Mkuu.

Katika hatua nyingine, Majaliwa amekiri kuwepo kwa viwanda vichache vya mbolea kunasababisha bei ya mbolea kupanda zaidi.

Amesema Serikali imeiona changamoto hiyo na imeshazungumza na wawekezaji kutoka Ujerumani ambao watajenga viwanda Kilwa na Mtwara ambapo vitaungana na kiwanda cha Minjingu na mbolea itazalishwa kwa wingi na kupunguza bei.

Majaliwa alikuwa akijibu swali la Neema Mgaya (Viti Maalum-CCM) aliyetaka kujua nini mkakati wa Serikali kuongeza uzalishaji wa mbolea ambapo asilimia 90 inatoka nje.

Chanzo: mwananchi.co.tz