Mwanza. Serikali ya Tanzania inatekeleza mikakati itakayofanikisha lengo la kuongeza idadi ya watalii kutoka zaidi ya milioni 1.5 kwa mwaka hadi milioni 10.
Hayo yameelezwa leo Alhamisi Desemba 12, 2019 na Rais John Magufuli wakati akifungua mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM jijini Mwanza.
Rais Magufuli ametaja mikakati hiyo kuwa ni kuboresha miundombinu ya usafirishaji na kuvitangaza zaidi vivutio vilivyopo nchini.
“Idadi ya watalii wanaotembelea nchini itakuwa moja ya vigezo na vipimo vya utendaji na ufanisi wa mabalozi wetu wanaotuwakilisha nje,” amesema mwenyekiti huyo wa CCM.
Kuhusu usafirishaji, Rais Magufuli ametaja sekta ya reli, barabara, anga na maji kuwa miongoni mwa maeneo yanayoendelea kuboreshwa kuhakikisha yanafikika kirahisi.
Amesema Serikali itahakikisha miundombinu ya reli inafika kila pembe ya nchi na nchi jirani za DRC, Burundi na Rwanda.
Mkuu huyo wa nchi ametaja na kusifia uamuzi wa Serikali ya Zanzibar (SMZ) kununua meli mpya akisema ni kati ya mikakati inayofanywa na Serikali zote mbili kuhakikisha inashika na kutawala njia za usafirishaji katika maziwa na bahari kuu.