Dar es Salaam. Rais John Magufuli amelitaka Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) kutobweteka baada ya kupata mafanikio makubwa.
Amesema kama TTCL itajiona imefanikiwa na kuendelea kubweteka, itajikuta ikitoka katika reli na kupoteza mafanikio yake.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo Juni 21 wakati akipokea gawio la Sh1.5 bilioni kutoka shirika hilo.
“Nawapongezeni sana kwa mafanikio haya mliyopata katika kipindi cha miaka miwili, hongereni sana. Lakini hata hivyo itakuwa ni jambo la aibu sana kama mafanikio mliyopata yakawafia mikononi,” amesema.
Rais amesema pamoja na mafanikio hayo pia waangalie namna ya kuendelea kuboresha huduma na kuangalia njia nyingine za kujiongezea kipato.
“Pia angalieni uwezekano wa kupunguza gharama ili muendelee kupata wateja zaidi,” amesema.