Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Magari kutumia stika za bima kielektroniki

211cb2c58b8abb14cf9039316d6dc634 Magari kutumia stika za bima kielektroniki

Fri, 20 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA) kuanzia Januari mwakani inatarajia kuanza kutumia mifumo ya Tehama kukusanya na kusimamia mapato yatokanayo na huduma za bima na pia kubaini waliolipa bima za magari.

Katika mfumo huo kwenye magari kutakuwa na stika za kielektroniki na malipo yatafanyika kielektroniki ili kuiwezesha Tira ifahamu idadi ya bima zilizolipwa kwa siku na kusajili ajali baada ya Polisi kuunganishwa kwenye mfumo.

Kamishna wa Bima, Dk Mussa Juma alisema jana kuwa, wanatarajia mifumo hiyo itarahisisha ukusanyaji mapato, taarifa na usimamizi kwa ujumla.

Akizungumza wakati wa kufungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo alisema katika kutekeleza majukumu yake ya kusimamia sekta, Tira inafuata miongozo na kanuni za utendaji kama inavyoelezwa na serikali.

Alisema miongozo hiyo ni pamoja na Mpango Mkakati wa Miaka wa Mitano 2018/19 -2022/23 (CSP), Mpango Kazi wa Mwaka Mmoja ambayo hutekelezwa na Mpango wa Bajeti (MTEF) ya kila mwaka wa fedha.

Kwa kuzingatia miongozo hiyo, katika kipindi cha mwaka uliopita 2019 sekta ya bima iliandikisha tozo ghafi za bima kiasi cha Sh bilioni 813.761 na katika mwaka huu Januari mpaka Juni, sekta imeweza kuandikisha tozo ghafi za bima lenye thamani ya Sh. bilioni 433.336.

Pamoja na tozo ghafi za bima kuongezeka kila mwaka, Tira bado imejiwekea malengo na mikakati ya kukuza soko la bima kwa huduma za bima kutoka asilimia 15 mpaka 50, kuongeza idadi ya mikataba ya bima inayokatwa kwa mwaka kutoka asilimia 20 mpaka 60.

Lengo lingine ni kuhakikisha wananchi wengi wanakuwa na uelewa wa huduma za bima kufikia asilimia 80 ifikapo Mwaka 2030.

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dotto James, akifungua mkutano huo alisema wizara imezindua Mpango wa Ukuzaji Sekta ya Fedha wa miaka kumi, 2020-2030, ambao umejumuisha sekta zote za fedha na bima.

Kwa mujibu wa mpango huo, Tira inapaswa kuhakikisha inafikia malengo kadhaa iliyowekewa katika mpango huo, ikiwa ni pamoja na kuwa idadi ya asilimia 50 ya watanzania wanafikiwa na huduma za bima kufikia Mwaka 2030 kutoka asilimia 15 ya sasa.

Pia alibainisha kuhakikisha kuongeza pato ghafi la bima za maisha kutoka asilimia 0.1 mpaka asilimia 03 na pato ghafi la bima za kawaida kukua kutoka asilimia 0.4 mpaka asilimia 2 kufikia Mwaka 2030.

Katika hotuba yake iliyosomwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Mipango katika Wizara ya Fedha, Theresia Henjewele alisema mamlaka ya bima kwa kushirikiana na wadau wengine wa sekta ya afya wanapaswa kuhakikisha asilimia 90 ya Watanzania wanakuwa na bima ya afya.

“Mamlaka inatakiwa kuhakikisha kuna njia mpya na rahisi za kusambaza huduma za bima kwa kuhuisha mifumo ya Tehama ili kupata taarifa na takwimu sahihi kwa wakati kwa maendeleo ya soko la bima”alisema

Aliwaagiza wajumbe wa baraza kupitia na kutekeleza bila kusahau kuwa sehemu kubwa ya watanzania wanategemea kilimo na Biashara ndogondogo, ni mategemeo ya Wizara kuwa kufikia Mwaka 2030, asilimia 10 ya pato ghafi la soko la bima litatokana na kinga katika sekta ya kilimo.

Alitoa maelekezo kwa menejimenti ya Tira na wafanyakazi wake kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha kuwa sekta ya bima inaongeza mchango wake kwenye Pato la Taifa, kutoka asilimia 0.53 hadi kufikia asilimia 3 ifikapo mwaka 2030.

Chanzo: habarileo.co.tz