Naibu Waziri wa Madini, Dk Steven Kiruswa amewaonya madalali wanaojihusisha na biashara ya madini kuacha mara moja kununua madini kwa wachimbaji wadogo chini ya bei elekezi na atakayebainika atawajibishwa.
Dk. Kiruswa ametoa maelekezo hayo akiwa ziarani mkoani Geita alipoambatana na Balozi wa Tanzania Nchini Zimbabwe pamoja na Naibu Waziri wa Madini waliokuja kujionea shughuli za wachimbaji wadogo.
Amesema serikali imeshatunga taratibu, kanuni na sheria zinazoongoza biashara ya madini na kuweka bei elekezi ambapo mnunuzi yeyote hatakiwi kununua chini ya bei hiyo, hivyo kwa madalali waonunua madini wazingatie.
“Sisi tumewasaidia watanzania kwa kuwawekea bei elekezi, bei elekezi ya dhahabu imepangwa kulingana na viwango vya soko la dunia, na bei elekezi tunayoweka sisi kama taifa ili wanaoununua na kuuza nao wapate kitu.
“Kwa hiyo unakuta kwamba bei iliyopo katika soko la dunia, kwa madini ya dhahabu ambayo tumeshuhudia hapa Geita imewekwa kwamba asilimia 10 ndiyo inaruhusu kumpa mfanyabiashara wa kati nafasi naye ya kununua kwa yule anayekuja kuuza.
“Sasa nitoe wito basi, kwa wale wafanyabiashara wa kati wanaojaribu kuwaomba wanaouwauzia washushe chini ya bei elekezi ya serikali, kwamba jambo hilo haliruhusiwi, ni kinyume cha sheria, ni kinyume cha taratibu na kanuni zetu.”