Maboresho makubwa yaliyofanyika katika bandari ya Tanga yamewezesha kuzishawishi meli zilizokuwa zinatumia bandari shindani za nchi jirani kutumia bandari hiyo.
Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana baada ya kufanyika kwa maboresho hayo ni hatua ya kampuni ya usafirishaji ya Simba Terminals kuwashawishi Wafanyabiashara kutumia bandari ya Tanga kushusha mizigo kutoka Russia kuelekea Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Meneja wa kampuni ya Simba Terminals, Awadhi Masawe amesema ushawishi huo umewezesha tani elfu 49 za mizigo kushushwa bandarini hapo.
Baada ya maboresho hayo takribani meli kubwa 19 zimetia nanga katika bandari hiyo ya Tanga na katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 mizigo yenye jumla ya uzito wa tani Milioni 1.2 itahudumiwa bandarini hapo.