Dar es Salaam. Laini za simu milioni 35.8 kati ya milioni 43 zimeshajiliwa kwa alama za vidole hadi kufikia Machi 10, 2020.
Hayo yameelezwa leo Ijumaa Machi 13, 2020 na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), James Kilaba katika maadhimisho ya siku ya kimataifa ya haki ya mteja.
Kilaba amesema idadi hiyo ni sawa na asilimia 83.1 ya laini zote, ni wazi kuwa zoezi la usajili wa laini za simu kwa alama za vidole limekuwa na manufaa.
“TCRA iliasisi mpango wa kusajili laini za simu kwa kutumia alama za vidole mwaka 2018, zoezi hili limekuwa lenye manufaa na kupata mwitiko mkubwa.”
“Hadi kufikia Machi 10, 2020 idadi ya laini zilizounganishwa mitandanoni ni 43,072,868 huku idadi ya laini zilizosajiliwa kwa alama za vidole ni 35,813,455 sawa na asilimia 83.1 ya laini zote,” amesema Kilaba.
Amesema lengo la usajili wa kutumia mfumo huo ni kuimarisha usalama katika matumizi ya simu za mkononi , kulinda watumiaji na kufanikisha shughuli nyingine za usimamizi.
Pia Soma
- Upelelezi kesi ya Shamimu na mumewe wakamilika
- Simbachawene asema Andengenye hakuwa na sifa kuingia mkataba wa Sh1 trilioni
- Mbowe alipa faini, muda wowote kutoka jela
Akizungumzia kuhusu siku ya haki ya mteja, Kilaba amesema siku hiyo huadhimishwa kila Machi 15 na maadhimisho ya mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiyu ya ‘Mteja Endelevu’.
“Kauli mbiu inajikita katika kusisitiza umuhimu wa upatikanaji wa huduma endelevu nasi katika sekta ya mawasiliano tumekuwa tukilitekeleza hilo, tunalitekeleza na tutaendelea kulitekeleza wakati wote,” amesema.
Katika maadhimisho hayo TCRA imekuwa ikifanya mikutano mbalimbali na wadau kwa muda wa wiki nzima wakitoa elimu ya mawasiliano katika shule na vyuo mbalimbali katika mikoa ya Shinyanga, Tabora, Arusha, Zanzibar na Pwani.