Mbunge wa Jimbo la Mlimba mkoani Morogoro, Godwin Kunambi ameiomba Serikali ije na mabadiliko ya sheria ya Shirika la Reli Tanzania na Zambia (TAZARA) kutokana na kuwepo kwa changamoto ya sheria hasa katika eneo la uwekezaji wa mtaji, kwa kuweka mgawanyo wa hisa kwa wawekezaji wa mitaji mikubwa ili wawe na hisa kubwa.
Kunambi amesema hayo leo Bungeni jijini Dodoma wakati akichangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha wa 2024/2025.
“Labda watu hawafahamu umuhimu wa reli ya TAZARA, ilianzishwa kwa sababu ya kurahisisha usafiri wa reli kutoka bandari ya Dar es Salaam kwenda Kapiri Mposhi, ilisaidia kuunganisha mahusiano ya kibiashara baina ya nchi zetu (Tanzania na Zambia),” amesema Mbunge Kunambi