NAIBU Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Kundo Mathew amemfuta kazi Meneja wa Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) Mkoa wa Kagera, Irene Shayo kwa kile kilichobainika kuwa taratibu za uteuzi wake zilikiukwa na utumishi wake umekuwa wa kusuasua.
Kundo amesema meneja huyo amekuwa akikwepa ziara za viongozi katika eneo lake pamoja na kupika taarifa za mapato na matumizi.
“Ninaagiza Meneja wa Mkoa wa Kagera aondoshwe mara moja katika Mkoa wa Kagera na kuanzia leo asitambulike kama Meneja wa Mkoa wa Kagera, taratibu zifuatwe na apangiwe kazi zingine kulingana na wasifu wake kitaaluma ili aweze kufanya kazi vizuri kwasababu majukumu ya sasa hana uwezo nayo”, alizungumza Mhandisi Kundo wakati wa ziara yake Mkoani Kagera