Biashara

Habari

Burudani

Michezo

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Kiwanda cha sukari cha Mkulazi yaingiza shehena za sukari mtaani

Kiwanda Cha Sukari Cha Mkulazi Kiwanda cha sukari cha Mkulazi yaingiza shehena za sukari mtaani

Fri, 9 Feb 2024 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Kiwanda kipya cha Sukari cha Mkulazi kilichopo wilayani Kilosa, Morogoro kimeingiza rasmi sheheza za bidhaa ya sukari kwa matumizi ya majumbani kwa mara ya kwanza tangu kuanza uzalishaji wenye lengo la kupunguza makali ya bei za sukari yanayowakabili wananchi katika Maeneo mbalimbali nchini.

Afisa Mwandamizi wa Masoko na Mauzo kutoka kampuni hodhi ya Mkulazi, Milkasia Joseph Mnkeni amebainisha hayo wakati wa zoezi la upakiaji wa sukari ya ujazo wa kilogram 25 ambayo imeanza kuingizwa rasmi sokoni kwa mkoa wa Morogoro.

Milkasia alisema Sukari hiyo imekidhi viwango vya ubora wa hali juu baada ya bidhaa hiyo kupitishwa katika vipimo vyote kwa ajili ya matumizi ya kawaida ambayo imelengwa kwa matumizi mbalimbali ikiwemo kiungo katika aina mbalimbali za mapishi yanayotajwa kwenda kuwafurahisha watumiaji wa sukari hiyo sokoni.

“Tumeanza zoezi la kuuza sukari, na kuanza kupakia kwenye magari ya wateja ambayo yamefika kiwandani kwetu leo, kwa sasa tayari tumeshaainisha wateja wetu, tunawakaribisha wafanyabiashara kufanya kazi na sisi, kuingiza sukari yenye ubora wa hali ya juu wa hali ya juu sokoni, kwa ajili ya kuisadia nchi yetu na kupunguza nakisi ya sukari,” alisema Milkasia.

Naye Afisa Uhusiano wa Kampuni hodhi ya Mkulazi, Clementina Patrick alisema wamejipanga vyema kuhakikisha bidhaa hiyo inawafikia watanzania wote kwa bei elekezi za serikali ili kuwapunguzia watumiaji wa bidhaa hiyo machungu kutokana na mfumuko wa bei uliosababishwa na uhaba wa sukari mtaani.

“Kama mnavyoona leo ndio siku ya kwanza tunaingiza bidhaa yetu ya sukari sokoni, kwa sasa tumeanza na sukari ya majumbani (brown sugar) na tunatarajia hapo baadae kuzalisha pia na sukari za viwandani, Sukari yetu tumeiuza kwa bei elekezi kwa wafanyabiashara, pia tunatarajia itawafikia watanzania kwa bei elekezi ya serikali ili kuwapunguzia wananchi makali,” alisema Clementina.

Kwa upande wake Meneja wa Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi, Mhandisi Aaron Mwaigaga, alisema kiwanda hicho kinaendelea na zoezi la uchakataji wa sukari ili kuendelea kuunga mkono jitihada za serikali kupunguza uhaba wa bidhaa hiyo mtaani unaosababishwa na mvua zinazondelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini.

Mhandisi Mwigaga alisema, Mkulazi imejidhatiti kuendelea kupeleka sukari sokoni licha ya changamoto za mvua zinazoendelea lakini pale hali ya hewa inapotulia watajitahidi kuendelea na zoezi la uchakataji wa sukari ili kupunguza nakisi ya sukari kwa wananchi kama ambavyo malengo ya serikali yalivyo katika kupunguza makali ya bei kwa jamii.

Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi ni kiwanda kipya kikimilikiwa kwa ubia wa hisa 96% kutoka kwa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na hisa 4% zikimilikiwa na Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Magereza (SHIMA) huku kikianza Uzalishaji wa majaribi ya sukari yake mwezi Desemba 2023.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live