Rufiji. Mkuu wa Mkoa wa Pwani nchini Tanzania, Everist Ndikilo amewataka wananchi kushirikiana na wawekezaji ili kuwa mabalozi wa kuvutia uwekezaji nchini.
Ndikilo ametoa kauli hiyo leo Jumanne Agosti 27, 2019 katika uzinduzi wa kiwanda cha kuchakata betri za magari zilizotumika cha Huatan Investment kilichopo kijiji cha Nyamwange Wilaya ya Rufiji.
"Tukiwapa ushirikiano wawekezaji wetu wataleta wengine. Tuwe na matumizi bora ya ardhi, mkulima akae eneo lake na mfugaji akae eneo lake.”
“Maeneo ya wawekezaji nayo tuyaache wakija kuwekeza msiwauzie kwa bei ya kuwaumiza iwe ina manufaa kwa pande zote," amesema.
Amebainisha kuwa kuna wawekezaji kutoka Uarabuni wanataka kuwekeza katika kiwanda cha sukari kitakachotoa ajira kwa watu wengi zaidi.
Meneja wa Kituo cha Uwekezaji (TIC) kanda ya Mashariki, Venance Mashiba amesema uwekezaji huo ulipitia katika kituo hicho mwaka 2017 na gharama ya uwezeshaji ilitajwa kuwa ni Dola 630,000 za Marekani sawa na Sh1.5 bilioni.
Pia Soma
- Mbarawa azindua bodi Tanga-Uwasa, aipa majukumu manne
- Wanawake watakiwa kuwa wamoja, kushirikiana
- Alichokisema mtumishi wa Tanesco kesi ya Gugai
"Kwa kuanza tutakuwa tukisafirisha malighafi kwenda nje ya nchi zinazotokana na betri zilizochakatwa kwa ajili ya kutengeneza betri mpya.”
“Lakini baada ya mwaka mmoja mpaka miwili ijayo kulingana na ustawi wa biashara tutaanza kuwa tunachakata na kutengeneza betri Tanzania kwa ajili ya soko la ndani," amesema Ding.