“Napenda kulifahamisha bunge lako tukufu kwamba nchi yetu ni miongoni mwa nchi zilizobarikiwa kuwa na madini mkakati ambayo uhitaji wake ni mkubwa kwenye nishati safi na salama na teknolojia nyingine za kisasa duniani. aidha, uhitaji huu unatokana na utekelezaji wa azimio la pamoja la dunia la kupunguza hewa ya ukaa ifikapo 2050 (Net Zero Emission), miongoni mwa madini mkakati yanayopatikana nchini ni pamoja na lithium, cobalt, nikeli, shaba, aluminium, zinki, kinywe na madini adimu (Rare earth elements-REE)"
"Mheshimiwa Spika (Dkt. Tulia Ackson) ili nchi yetu iweze kunufaika na madini hayo, wizara imeandaa mkakati wa uendelezaji wa madini muhimu na madini mkakati hapa nchini. Mkakati huo unalenga kuhakikisha kwamba madini hayo yanaongezwa thamani hapa nchini ikiwamo kuzalisha bidhaa zinazohitajika katika soko kama vile betri za magari ya umeme na hivyo kuongeza manufaa kwa nchi ikiwamo kuongeza mapato ya Serikali na ajira kwa watanzania, ili kuongeza manufaa yatokanayo na madini muhimu na madini mkakati, kwa mara ya kwanza kitajengwa kiwanda kikubwa na cha kisasa cha usafishaji na uongezaji thamani madini cha Multi Metals Processing Facility katika eneo maalumu la ukanda wa kiuchumi la Buzwagi Special Economic Zone lililopo Wilaya ya Kahama”- Mavunde.
Waziri wa Madini Anthony Peter Mavunde akiwasilisha bungeni Makadirio ya Mapato na Matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2024/2025, siku ya Jumanne Aprili 30, 2024.