Shirika la Umeme (Tanesco) limeeleza jinsi kituo cha kupokea na kupoza na kusambaza umeme cha Mpomvu mkoani Geita kitakavyoongeza upatikanaji wa nishati ikiwa pamoja na kufanikisha uchimbaji wa dhahabu.
Kituo hicho kilichozinduliwa leo Jumamosi, Oktoba 15, 2022, Rais Samia Suluhu Hassan kinatarajiwa kuondoa changamoto ya mahitaji makubwa ya umeme kutoka mahitaji ya megawati nne za mwanzo kufikia mahitaji ya megawati 18 za sasa.
Akitoa taarifa ya mradi huo kwa Rais Samia, Mkurugenzi wa Tanesco, Maharage Chande amesema mahitaji yaliongezeka na kusababisha shirika hilo kushindwa kutoa huduma kwa wateja wao ambao ni Mgodi wa dhahabu Geita (GGM), kiwanda cha kusafisha dhahabu na wachimbaji wadogo.
“Kituo cha mradi huu kina sehemu tatu, sehemu ya kwanza ni kujenga njia kubwa kutoka Bulyanhulu Shinyanga (mkoa wa Shinyanga) mpaka hapo (kituo kilipo) ina uwezo wa kuleta umeme megawati 200 badala ile ya mwanzo megawati nne,” amesema
Amesema sehemu ya pili ya mradi ni kujenga mashine za kupooza umeme mkubwa kisha kusambazwa kituoni hapo akidai mashine zilizowekwa zina uwezo wa kupooza mpaka megawati 90 za umeme.
“Kwa hiyo kwenye mahitaji ya megawati 18 za sasa tuna nafasi ya kama megawati 72 kwenye hii miundombinu kwa ukuaji wa baadaye,” amesema Chande
Amesema sehemu ya tatu ya mradi huo unaogharimu dola za kimarekani 23 milioni ni kusambaza umeme vijijini na kuongeza kuwa mapato ya shirika hilo yataongezeka kufikia Sh6 bilioni huku mgodi wa GGM kuokoa Sh4 bilioni ambazo zinatumika kununua mafuta ya kuendeshea mgodi huo.
“Mashine umba zinazoshusha umeme mkubwa wenye megawati 220 kufikiamegawati 33 tulizozigawanya hapa Geita na sehemu nyingine ambapo hapa kuna mgawanyo matoleo yapo saba kwenda sehemu mbalimbali.
“Kwa mfano toleo moja litakwenda GGM ambao tumeshasaini nao mkataba. Kuanzia Machi mwaka ujao mapato ya shirika yataongezeka kwa mwezi kama Sh6 bilioni na wao (GGM) watasave (wataokoa) Sh4 bilioni,” amesema.